Chanongo aing'arisha Mtibwa Sugar
Muktasari:
Kagera Sugar walikuwa wa kwanza katika mchezo huo kupata bao la kuongoza kupitia kwa Awesu Awesu kabla ya Juma Nyoso kuisawazishia Mtibwa Sugar kwa kujifunga huku mengine ya ushindi yakifungwa na Chanongo.
KOCHA wa Mtibwa Sugar, Zubeir Katwila amesema ubora wa winga wake, Haruna Chanongo ulikuwa sehemu ya matokeo mazuri waliyoyapata ugenini katika mchezo uliopita wa Ligi Kuu Bara dhidi ya Kagera Sugar.
Katika mchezo huo, uliochezwa Uwanja wa Kaitaba mjini Bukoba, Chanongo ambaye aliwahi kuzichezea Simba na Stand United, alipachik a mabao mawili katika ushindi wa mabao 3-1.
Katwila ambaye alikuwa kocha bora mwezi uliopita Oktoba katika ligi, alisema ni mategemeo yake kumuona Chanongo akiendelea kufanya vizuri kikosini kutokana na mchezaji huyo kuwa na kipaji.
“Ni kati ya wachezaji muhimu kwenye kikosi changu, alicheza kwa kujituma na ninaamini kile kiwango kitaendelea katika michezo mingine, hakuna kinachoweza kumbana asionyeshe makali yake, nimekuwa nikikaa naye kama mwalimu,” alisema kocha huyo.
Hata hivyo, Mtibwa Sugar ambao wapo nafasi ya tano kwenye msimamo wa ligi, hawakuwa na mwanzo mzuri wa msimu baada ya kuvurunda michezo yao mitano.
Waliuanza msimu Agosti 25 kwa kukumbana na kipigo cha mabao 3-1 dhidi ya Lipuli, Septemba 13 walipigwa na Simba mabao 2-1, Septemba 21 wakatoka suluhu dhidi ya JKT Tanzania.
Septemba 25, Mtibwa Sugar wakiwa nyumbani walikubali kipigo cha mabao 3-1 dhidi ya Tanzania Prisons, Septemba 29 walitoka sare ya bao moja na Mbeya City hivyo katika michezo hiyo, waliambuliwa pointi mbili pekee.