Buswita arejea mzigoni na malengo kibao

Muktasari:

Pamoja na kwamba Pius Buswita amekaa nje nusu msimu baada ya kuachwa na Yanga, amefichua jambo kwamba hakujibweteka na ataanza majukumu na Polisi Tanzania akiwa kwenye kiwango.

MCHEZAJI mpya wa Polisi Tanzania, Pius Buswita amesema hakujibweteka baada ya kuachana na Yanga kwamba aliendelea na programu zake za mazoezi, anayoamini yatamuweka kwenye kiwango kizuri atakapoanza majukumu rasmi.
Buswita amesaini mkataba wa mwaka mmoja na Polisi Tanzania, jambo analojivunia na kwamba anarejea kwenye majukumu yake baada ya kukaa nje nusu msimu.
Amesema kazi yake ni soka, ikitokea anakosa majukumu ya kufanya kinakuwa ni kitu cha maumivu kwake, hivyo kupata timu anaona ni muda wake wa kuonyesha kipaji chake.
"Kazi yangu ni soka inapotokea sina timu si rahisi kuwa na furaha, nashukuru Mungu naamini kupitia Polisi Tanzania nitafanya kitu cha tofauti,"
"Licha ya kwamba sikuwa na timu ya kucheza, niliendelea na programu zangu za mazoezi kuuweka mwili wangu fiti, naamini sitakuwa mzigo wa kuanza moja,"amesema.
Yanga iliachana na Buswita msimu huu ambapo hakuwa na nafasi kwenye kikosi cha kwanza cha kocha Mwinyi Zahera.