Azam FC , Kagera gari limewaka

Muktasari:

Kikosi cha Azam Fc kimeendeleza ushindi mfululizo baada ya kushinda mechi zake mbili za ugenini mkoani Mwanza.

AZAM FC jana Jumanne iliichapa Alliance 5-0 mchezo uliopigwa Uwanja wa Nyamagana jijini Mwanza na ushindi huo unakuwa mkubwa kwa mara ya kwanza kwenye kikosi hicho kinachonolewa na Aristica Cioaba.

Ushindi huu unaifanya Azam kushika nafasi ya nne wakiwa na pointi 19 katika mechi tisa walizocheza mpaka hivi sasa kwenye ligi.

Azam imejikusanyia pointi sita wakiwa Mwanza  baada ya kushinda 1-0 dhidi ya Mbao na Alliance huku mshambuliaji wao Obrey Chirwa akifunga hat trick yake ya kwanza msimu huu.

Kagera Sugar wanashika nafasi ya pili kwenye msimamo wa ligi kuu wakicheza mechi 12 na kukusanya pointu 23 huku Simba ikiwa kileleni kwa pointi 25.

Mchezo mwingine ulioteka hisia ulikuwa ni Mbao dhidi ya KMC ambapo Mbao inayofundishwa na Hemed Morocco ilishinda bao 2-0.

Ukiachana na michezo hiyo, Novemba 29 Alliance watakuwa na kibarua kingine mbele ya  Yanga mchezo utakaopigwa Uwanja wa CCM Kirumba, Mwanza.

Yanga katika mchezo wao dhidi ya JKT Tanzania walishinda 3-2 huku Alliance wakifungwa bao 5-0 na Azam Fc, hivyo kila timu inahitaji ushindi katika mchezo huo.