Ronaldo: Huyo Messi nimembana kona hii

Muktasari:

Barcelona hawapo tayari kutoa kiasi cha Pauni 200 milioni ambazo PSG wanazihitaji kwa kuwa katika siku za karibuni wamelipa kiasi cha Pauni 108 na kumnasa Antoine Griezmann

MADRID, HISPANIA . NYOTA wa Juventus Cristiano Ronaldo kaibuka na kutaja eneo moja tu ambalo amemzidi mhasimu wake Lionel Messi anayekipiga Barcelona.
Ronaldo amesema kuwa Messi ni mchezaji mzuri na ndio maana data zao zinakimbizana lakini amemzidi kwa kucheza katika timu tofauti ambazo zimeshiriki Ligi ya Mabingwa Ulaya na nyingine kupata medali. 
Kumekuwa na malumbano kadhaa juu ya nani ana kiwango kati ya Ronaldo na Messi na mchezaji huyo wa Ureno ameibuka na kujipa ujiko.
Wakati Messi akitumia maisha yake ya soka Barcelona,    Ronaldo amepita katika klabu kubwa kama Sporting Lisbon, Manchester United , Real Madrid na sasa Juventus.
Ronaldo alipata ubingwa wa Ligi ya Mabingwa Ulaya akiwa na Man United mwaka 2008 na akiwa Real Madrid alipata ubingwa huo mara nne.
“Tofauti yangu na Messi ni kwamba nimecheza katika ligi mbalimbali na kupata ubingwa wa Ligi ya Mabingwa Ulaya na timu tofauti,” alisema.
“Nilikuwa mfungaji bora wa Ligi ya Mabingwa Ulaya mara sita mfululizo. Vile vile nimepata ubingwa wa Ligi ya Mabingwa mara tano. Ni wachezaji wachache ambao wameweza kufikia kiwango hicho.”