Wakala wa Saliba aomba kikao Arsenal
Muktasari:
- Saliba ambaye ni beki tegemeo wa timu ya taifa ya Ufaransa, mkataba wake katika viunga vya Emirates unamalizika mwaka 2027 na Madrid ipo tayari kujadiliana kuhusu kumnunua ifikapo mwisho wa msimu ujao au ikiwezekana hata katika dirisha dogo.
LONDON, ENGLAND: WAKALA wa beki kisiki wa Arsenal, William Saliba ametuma ombi la kukutana haraka na mabosi wa Arsenal ili kujadili mkataba mpya katika nyakati hizi ambazo Real Madrid imeonyesha kuongeza dhamira ya kutaka kumsajili mwakani.
Saliba ambaye ni beki tegemeo wa timu ya taifa ya Ufaransa, mkataba wake katika viunga vya Emirates unamalizika mwaka 2027 na Madrid ipo tayari kujadiliana kuhusu kumnunua ifikapo mwisho wa msimu ujao au ikiwezekana hata katika dirisha dogo.
Tovuti ya Diario AS inaeelza, Madrid inaangalia kwa makini hali ya Saliba na Arsenal kwa sababu wanamwona beki huyo kama mpango wao wa muda mrefu.
Madrid huenda ikaachana na David Alaba na Antonio Rudiger katika dirisha lijalo la majira ya kiangazi kutokana na umri wao pamoja na ofa ambazo wanadaiwa kuzipata kutoka Saudi Arabia, hivyo Saliba anaonekana kama mbadala sahihi wa kucheza beki wa kati baada ya wakongwe hao kuondoka.
Hadi sasa Saliba hajasaini mkataba mpya Emirates na Madrid imekuwa ikizungumza sana na mawakala wake ambao wamewapigia simu mabosi wa Arsenal na kuwaomba kukutana haraka kujua kiasi gani ambacho wanaweza wakatoa ili kuona kama wataendelea kufanya mazungumzo na Madrid au wataachana nao na beki huyo asaini mkataba mpya.
Saliba mwenyewe yupo tayari kusaini mkataba mpya lakini anataka ongezeko la mshahara linalodaiwa kufikia mara mbili ya ule ambao anaupata kwa sasa.
Madrid pia imemjumuisha beki wa Liverpool, Ibrahima Konate, katika orodha ya mabeki wa kati inaowawinda na huenda ikaanza na Mfaransa huyo kwanza kwani mkataba wake unamalizika mwisho wa msimu huu.
Kwa sasa Saliba bado anaendelea kufanya mazoezi ili kujiweka sawa zaidi baada ya kupata jeraha la kifundo cha mguu katika mechi ya Ligi Kuu England dhidi ya Liverpool.