Toni Kroos kufuata nyayo za Zidane Real Madrid
Muktasari:
- Kroos (36), alihitimisha safari yake ya soka la ushindani mwishoni mwa michuano ya Euro 2024, akiondoka Real Madrid kama mmoja wa wachezaji wenye mafanikio makubwa zaidi katika historia ya klabu hiyo.
MADRID, HISPANIA: KIUNGO gwiji wa zamani wa timu ya taifa ya Ujerumani, Toni Kroos, anaripotiwa kuwa mbioni kurejea kwa hisia ndani ya klabu ya Real Madrid ikiwa ni miezi michache tangu atangaze kustaafu soka.
Kwa mujibu wa taarifa kutoka The Athletic, Kroos yuko kwenye mazungumzo na mabingwa hao wa kihistoria wa La Liga kuhusu kuchukua nafasi mpya ndani ya uongozi wa klabu hiyo yenye majukumu mazito.
Kroos (36), alihitimisha safari yake ya soka la ushindani mwishoni mwa michuano ya Euro 2024, akiondoka Real Madrid kama mmoja wa wachezaji wenye mafanikio makubwa zaidi katika historia ya klabu hiyo.
Tangu kustaafu kwake, amekuwa akielekeza nguvu zake kwenye kituo chake cha kukuza vipaji, Toni Kroos Academy, kilichozinduliwa rasmi Septemba 2024.
Inaelezwa kuwa, uongozi wa Real Madrid una shauku ya kumjumuisha Kroos kwenye muundo wao wa kiufundi na michezo (sporting structure). Mpango huo unafananishwa na njia aliyopita mkongwe mwingine, Zinedine Zidane.
Itakumbukwa kuwa Zidane alianza kama mshauri wa klabu mnamo Novemba 2010, akajifunza mifumo ya uongozi, kabla ya kuja kuwa kocha mkuu na kuipatia timu hiyo mafanikio makubwa, ikiwemo mataji matatu mfululizo ya Ligi ya Mabingwa (UEFA Champions League).
Habari hizi zimeleta msisimko mkubwa kwa mashabiki wa ‘Los Blancos’ ambao bado wanaamini busara na uzoefu wa Kroos ni muhimu katika kipindi hiki ambacho timu inapita kwenye mabadiliko ya kizazi.
Ikiwa makubaliano yatafikiwa, Kroos ataanza sura mpya ya maisha yake ya soka nje ya uwanja, akisaidiana na rais Florentino Perez na benchi la ufundi kuendeleza ukubwa wa klabu hiyo.