Saka: Arsenal kila siku inaonewa
Muktasari:
- Mwamuzi Jarred Gillett awali aliamua ilikuwa ni penalti, lakini baada ya muda akaenda kutazama katika VAR na alibadilisha uamuzi wake.
LONDON, ENGLAND: STAA wa Arsenal, Bukayo Saka ametoa maneno makali dhidi ya VAR baada ya Arsenal kunyimwa penalti kipindi cha kwanza, licha ya faulo ambayo straika wao, Viktor Gyokeres alifanyiwa na kipa wa Newcastle United, Nick Pope.
Mwamuzi Jarred Gillett awali aliamua ilikuwa ni penalti, lakini baada ya muda akaenda kutazama katika VAR na alibadilisha uamuzi wake.
Hata hivyo, Arsenal bado iliibuka na ushindi wa mabao 2-1 kwa bao la dakika za mwisho lililofungwa na Gabriel, lakini Saka alionyesha kutoridhishwa kwake na uamuzi wa kubatilisha penalti ya kipindi cha kwanza.
Katika mahojiano yake baada ya mechi, Saka alidai maamuzi ya aina hii kila mara huwa yanatokea kuwaumiza wao.
Marudio ya picha yalionyesha Pope alipiga mpira kidogo kabla ya kumwangusha Gyokeres jambo ambalo lilimwaminisha mwamuzi kuwa kipa huyo hakufanya faulo.
Hata hivyo, Arsenal inaamini mgusano uliotokea kati ya Pope na Gyokeres ulimyima mshambuliaji huyo nafasi ya kufunga bao jambo ilipaswa kumfanya mwamuzi aamue ilikuwa ni penalti.
Saka, aliyerejea kikosini baada ya kuwa nje kwa muda kutokana majeraha, aliisaidia Arsenal kubadilika kiuchezaji hata ikasawazisha na kuongeza bao la ushindi.
Ushindi huo uliipandisha Arsenal hadi nafasi ya pili kwenye msimamo wa ligi, ikiwa pointi mbili tu nyuma ya Liverpool, ambayo ilipoteza dhidi ya Crystal Palace Jumamosi.
"Ni mambo kama haya ambayo kila mara huwa yanatokea na kuyunyima nafasi, lakini leo tumepata tulichostahili na ndiyo maana wote tuna furaha. Sasa haijalishi tena ikiwa tulinyima penalti."