Saka afichua wasiwasi wake wakati akijiuguza

Muktasari:
- Winga huyo mwenye umri wa miaka 23 alilazimika kuwa nje ya uwanja kwa miezi mitatu msimu uliopita baada ya kufanyiwa upasuaji wa misuli ya paja wakati wa mkesha wa Krismasi.
LONDON, ENGLAND: STAA wa Arsenal, Bukayo Saka amefunguka athari alizokabiliana nazo kimwili na kiakili wakati alipokumbwa na majeraha makubwa yaliyoweka kwenye mashaka makubwa maisha yake ya soka.
Winga huyo mwenye umri wa miaka 23 alilazimika kuwa nje ya uwanja kwa miezi mitatu msimu uliopita baada ya kufanyiwa upasuaji wa misuli ya paja wakati wa mkesha wa Krismasi.
Staa huyo wa kimataifa wa England alikiri kuwa kwenye wasiwasi mkubwa kama angefanikiwa kurejea uwanjani na kucheza kwa makali kama mwanzo baada ya kufanyiwa upasuaji huo.
Saka alisema: “Siku mbili za kwanza zilikuwa ngumu - nilipofahamu tatizo gani linanikabili na natakiwa kufanyiwa upasuaji. Nilianza kuwaza, je nitakuwa kwenye kiwango changu?
"Wachezaji walirejea uwanjani baada ya kuumia na hawakuwa sawa kama mwanzoni. Lakini baada ya siku mbili, upasuaji ulifanyika kwa mafanikio na nilikuwa nasubiri kupona.”
Saka alifichua alihitaji muda mwingi wa kufikiria juu ya jambo hilo la upasuaji kabla ya kukubaliana na hali halisi, huku akifanya jambo hilo kwenye kipindi cha Krismasi.
Saka alirejea uwanjani mwanzoni mwa Aprili na kuitumikia Arsenal kwenye Ligi ya Mabingwa Ulaya na timu yake ikikomea kwenye hatua ya nusu fainali ikisukumwa nje na Paris Saint Germain.
Wasiwasi wa Saka ulikuwa kazi bure baada ya staa huyo kwa sasa kuendelea kucheza kwa kiwango chake akipewa nafasi pia ya kuitumikia timu yake ya taifa ya England chini ya kocha Thomas Tuchel.