Orlando Pirates yapindua meza, yang'oka Ligi ya Mabingwa Afrika
Muktasari:
- Orlando ilipoteza ugenini wikiendi iliyopita kwa idadi kama hiyo ya mabao 3-0 na ilipambana na kupindua meza na mechi kwenda katika penalti, lakini ikapoteza kwa mikwaju 5-4.
LICHA ya kulipa kisasi dhidi ya FC Lupopo ya DR Congo kwa kupata ushindi wa mabao 3-0 jioni hii katika pambano la marudiano la raundi ya pili ya Ligi ya Mabingwa Afrika, lakini vigogo hivyo vya soka vya Afrika Kusini vimeaga michuano hiyo.
Orlando ilipoteza ugenini wikiendi iliyopita kwa idadi kama hiyo ya mabao 3-0 na ilipambana na kupindua meza na mechi kwenda katika penalti, lakini ikapoteza kwa mikwaju 5-4.
Orlando ilionekana kama ingeweka rekodi ya kuwa klabu ya kwanza ya Sauzi kufungwa mabao 3-0 na kupindua dhidi ya wapinzani,lakini penalti ziliiangusha baada ya kukosa mbili kati ya sita ilizopita wakati Lupopo ikikosa moja ya kukwamisha tano wavuni.
Katika dakika 90 za pambano hilo Orlando iliandika bao la kwanza kupitia kwa Masindi
Namtajela dakika 39 lililodumu hadi mapumziko.
Kipindi cha pili, Yanela Mbuthuma iliandika bao la pili katika dakika ya 68 kabla ya Oswin Appollis kupigilia bao la tatu dakika ya 90+5na kufanya matokeo ya jumla kuwa mabao 3-3.
Orlando ilionyesha dalili mbaya katika hatua ya penalti baada ya mkwaju wa kwanza uliopigwa na Hotto kupotea maboya muda mchache baada ya Lupopo kufunga.
Kisha ikatulia na kutupia zikizofuata, wakati Lupopo ikipoteza penalti yao iliyokuwa ya nne na kufanya penalti tano tano ziishe kila moja kukwamisjha nne na wageni walifunga ya sita, huku Mbuthuma akikosa na kuitoa michuanoni Orlando na kuiacha Lupopo ikiungana na Al Hilal ya Sudan, Yanga ya Tanzania na Power Dynamos ya Zambia kutinga makundi ambapo droo ya hatua inatarajiwa kufanyika Novemba 3 huko Sauzi.