Odegaard awapa kicheko Arsenal, kukipiga na Spurs
Muktasari:
- Odegaard, 26, amekuwa nje ya uwanja tangu mwanzoni mwa Oktoba kutokana na kusumbuliwa na maumivu ya goti aliyopata kwenye mechi ya ushindi wa mabao 2-0 iliyopata Arsenal dhidi ya West Ham United.
LONDON, ENGLAND: NAHODHA wa Arsenal, Martin Odegaard amesema ameanza kupona majeraha yake hivyo matumaini yake ni makubwa atakuwapo kwenye mechi ya North London derby, Jumapili.
Odegaard, 26, amekuwa nje ya uwanja tangu mwanzoni mwa Oktoba kutokana na kusumbuliwa na maumivu ya goti aliyopata kwenye mechi ya ushindi wa mabao 2-0 iliyopata Arsenal dhidi ya West Ham United.
Kiungo huyo alikosa mechi tatu za mwisho za Norway za kufuzu Kombe la Dunia na taifa lake hilo limekamatia tiketi ya kucheza fainali hizo zitakazofanyika mwakani Amerika Kaskazini.
Katika kipindi cha mechi za kimataifa, Arsenal ilipata pigo jingine baada ya mabeki wake wawili Gabriel Magalhaes na Riccardo Calafiori kupata majeraha jambo linalowaweka kwenye hatihati ya kucheza mechi hiyo dhidi ya Tottenham.
Odegaard ameshakosa mechi 12 za Arsenal msimu huu, jambo lililomfanya kocha Mikel Arteta kufanya mabadiliko kadhaa kwenye safu ya kiungo ya kikosi chake. Kocha Arteta alibaki hana majibu wakati alipoulizwa kuhusu Odegaard, Kai Havertz, Noni Madueke, Viktor Gyokeres na Gabriel Martinelli kama watakuwapo uwanjani baada ya mapumziko ya mechi za kimataifa.
"Baadhi yao, wote hao, sifahamu," amesema Arteta kabla ya Arsenal kutoka sare na Sunderland.
"Kuna vitu vingi lazima vitokee katka wiki mbili zijazo, lakini nadhani wanakaribia na tutakuwa kwenye hali nzuri."
Lakini, kocha Arteta amepata presha nyingine kuhusu mabeki wake, licha ya kwamba kuna matumaini ya Calafiori kuwapo kwenye mechi ya Spurs, Gabriel bado ni utata kutokana na kusumbuliwa na maumivu ya paja, aliyopata kwenye mechi ya Brazil ya ushindi wa mabao 2-0 dhidi ya Senegal, iliyochezwa uwanjani Emirates.