Mourinho aichimba mkwara Chelsea, atamba kuinyamazisha
Muktasari:
- Chelsea itaikaribisha Benfica uwanjani hapo, ikiwa na kumbukumbu mbaya ya kupoteza mechi ya Premier dhidi ya Brighton mwishoni mwa wiki iliyopita, hali ambayo ilizua sintofahamu kwa mashabiki wa The Blues ambao wameonyesha kutopendezwa na matokeo hayo.
Kocha wa Benfica ya Ureno, Jose Mourinho ametamba kuinyamazisha Chelsea katika mechi ya Ligi ya Mabingwa Ulaya, itakayochezwa leo Septemba 30, 2025 kwenye Uwanja wa Stamford Bridge jijini London.
Chelsea itaikaribisha Benfica uwanjani hapo, ikiwa na kumbukumbu mbaya ya kupoteza mechi ya Premier dhidi ya Brighton mwishoni mwa wiki iliyopita, hali ambayo ilizua sintofahamu kwa mashabiki wa The Blues ambao wameonyesha kutopendezwa na matokeo hayo.
Mourinho amesema kwa sasa Chelsea haina makali kama miaka kadhaa iliyopita, hivyo atahakikisha kikosi chake kinatumia udhaifu huo kuibuka na ushindi utakaowapa pointi tatu.
Mourinho alitangazwa kuwa kocha mkuu wa Benfica wiki iliyopita baada ya kuachana na klabu ya Fenerbahçe ya Uturuki.
Mourinho amewahi kuinoa Chelsea katika vipindi viwili tofauti, mara ya kwanza ilikuwa 2004 hadi 2007, kisha 2013 hadi 2015.
Akiwa Chelsea, Mourinho alichukua taji la Premier mara tatu (2004–05, 2005–06 na 2014–15), FA mara moja (2006–07), Kombe la Ligi mara tatu (2004–05, 2006–07 na 2014–15) na Ngao ya Jamii mara moja (2005).
Ratiba ya Ligi ya Mabingwa Ulaya leo
Atalanta v Club Brugge
Kairat ve Real Madrid
Atletico Madrid v Eintracht Frankfurt
Bodø / Glimt v Tottenham Hotspur
Chelsea v Benfica
Galatasaray v Liverpool
Inter Milan v Slavia Prague
Marseille v Ajax
Pafos v Bayern Munich