Messi kubeba Ballon d’Or ya tisa?
Muktasari:
- Messi tayari amefunga mabao sita katika mashindano hayo na ameendelea kuvunja rekodi mbalimbali, jambo ambalo limemrudisha kwenye mjadala wa tuzo ya mchezaji bora duniani. Hata hivyo, kushinda Kombe la Dunia pekee hakutoshi.
MEXICO CITY, MEXICO: LIONEL Messi mshindi mara nane wa tuzo ya mchezaji bora Ulaya (Ballon d’Or), lakini wakati michuano ya Kombe la Dunia 2026 ikiendelea, swali kubwa linalozungumzwa na mashabiki wa soka duniani ni iwapo Lionel Messi anaweza kushinda Ballon d’Or ya tisa ikiwa ataiongoza Argentina kutetea taji la dunia.
Messi tayari amefunga mabao sita katika mashindano hayo na ameendelea kuvunja rekodi mbalimbali, jambo ambalo limemrudisha kwenye mjadala wa tuzo ya mchezaji bora duniani. Hata hivyo, kushinda Kombe la Dunia pekee hakutoshi.
Kwa mujibu wa historia ya Ballon d’Or, kutwaa Kombe la Dunia huongeza nafasi kubwa ya mchezaji kushinda tuzo hiyo, lakini siyo jambo linalohakikisha ushindi. Kabla ya 1995, wakati Ballon d’Or ilikuwa ikitolewa kwa wachezaji wa Ulaya pekee, ni wachezaji watatu tu walioweza kushinda Kombe la Dunia na Ballon d’Or katika mwaka mmoja ambao ni Bobby Charlton (1966), Paolo Rossi (1982) na Lothar Mattheus (1990).
Hata hivyo, baada ya tuzo kufunguliwa kwa wachezaji kutoka duniani kote, waliofanikiwa kufanya hivyo ni Zinedine Zidane (1998), Ronaldo de Lima (2002), Fabio Cannavaro (2006) na Lionel Messi (2022, alikabidhiwa tuzo mwaka 2023).
Historia inaonyesha siyo lazima bingwa wa dunia ashinde Ballon d’Or, lakini kuna mifano kadhaa ambapo mshindi wa Kombe la Dunia hakuchukua Ballon d’Or. Mwaka 2010, licha ya Hispania kutwaa Kombe la Dunia na Andres Iniesta pamoja na Xavi kuwa na msimu mzuri, Messi ndiye aliyeshinda Ballon d’Or kutokana na kiwango chake bora akiwa Barcelona.
Vilevile 2014, Argentina ilifika fainali ya Kombe la Dunia na Messi akang’ara, huku Manuel Neuer akiwa bingwa wa dunia akiichezea Ujerumani, lakini Cristiano Ronaldo ndiye aliyeshinda Ballon d’Or. Mwaka 2018, Luka Modric alitwaa Ballon d’Or baada ya kuiongoza Croatia hadi fainali ya Kombe la Dunia, akiwapiku hata baadhi ya mabingwa wa dunia wa Ufaransa.
MESSI ANAHITAJI NINI?
Iwapo Argentina itafanikiwa kutetea ubingwa wa Kombe la Dunia na Messi akaendelea kuwa mchezaji muhimu kwa mabao na mchango wake uwanjani, nafasi yake ya kushinda Ballon d’Or ya tisa itaongezeka kwa kiasi kikubwa. Hata hivyo, kura za Ballon d’Or huzingatia pia kiwango cha mchezaji katika msimu mzima, mafanikio ya klabu, mafanikio ya timu ya taifa na ushindani kutoka kwa nyota wengine.
Wachezaji kama Ousmane Dembele, Kylian Mbappe, Harry Kane, Cristiano Ronaldo na Vinicius Junior wanaweza pia kuingia kwenye kinyang’anyiro ikiwa wataendelea kufanya vizuri.
Historia inaonyesha wazi kuwa kushinda Kombe la Dunia ni faida kubwa katika mbio za Ballon d’Or, lakini hakuhakikishii ushindi. Ikiwa Messi ataiongoza Argentina kutwaa ubingwa na akaendelea kuwa mchezaji bora wa mashindano pamoja na kuwa na msimu bora kwa ujumla, atakuwa miongoni mwa wagombea wakuu wa Ballon d’Or 2026 na anaweza kuweka historia kwa kutwaa tuzo hiyo mara ya tisa.