Mashabiki West Ham wamshambulia David Sullivan
Muktasari:
- Mashabiki waliokuwa wamefurika kwenye Uwanja wa London waliimba nyimbo za kumkejeli Sullivan, jambo lililomfanya kuondoka mapema kwenye jukwaa la viongozi wakuu kabla ya mechi kuisha.
LONDON, ENGLAND: Mashabiki wenye hasira wa West Ham United wamemgeukia mmiliki mwenza wa klabu hiyo, David Sullivan, baada ya timu hiyo kushuka Ligi Kuu England hadi Championship.
Mashabiki waliokuwa wamefurika kwenye Uwanja wa London waliimba nyimbo za kumkejeli Sullivan, jambo lililomfanya kuondoka mapema kwenye jukwaa la viongozi wakuu kabla ya mechi kuisha.
Sullivan na aliyekuwa makamu wake, Karren Brady, wamekuwa wakikabiliwa na maandamano kutoka kwa mashabiki msimu mzima.
Licha ya West Ham kupata ushindi dhidi ya Leeds katika mchezo wa mwisho, bado walihitaji Tottenham ifungwe na Everton ili kujinusuru, jambo ambalo halikutokea.
Nahodha wa timu hiyo, Jarrod Bowen mwenye umri wa miaka 29, ameeleza kusikitishwa kwake na matokeo hayo akisema ni wakati mgumu sana kwa klabu kubwa kama hiyo kushuka daraja.
Bowen ameongeza kuwa japo kuna tetesi za yeye kuhitajika na Chelsea na Newcastle, lengo lake kwa sasa ni kuisaidia timu hiyo kurejea Premier League, ingawa klabu inalazimika kuuza wachezaji ili kupata zaidi ya Pauni milioni 100 kufuatia anguko hilo.
Kwa upande mwingine, kocha Nuno Espirito Santo amewaomba msamaha mashabiki na kueleza kuwa ulikuwa msimu wa ajabu kwani pointi 39 walizovuna hazikutosha kuwabakiza ligi kuu.
Licha ya uongozi wa West Ham kutaka kocha huyo mwenye umri wa miaka 52 abaki klabuni hapo, inasemekana anapanga kuondoka. Nuno amesisitiza kuwa jambo la muhimu kwa sasa ni klabu hiyo kupita katika kipindi hiki cha huzuni na kujipanga upya ili kurudi haraka kwenye ligi kuu ya England.