Lejendi Liverpool atoa onyo dili la Semenyo
Muktasari:
- Semenyo, mwenye umri wa miaka 26, anatarajiwa kujiunga na kikosi cha Pep Guardiola kwa ada ya Pauni 65 milioni ambayo iliwekwa kama bei katika mkataba wake kwa timu inayohitaji kuuvunja.
MANCHESTER, ENGLAND: LEJENDI wa Liverpool, Jamie Redknapp amesema staa wa Bournemouth, Antoine Semenyo bado anaweza kujiunga na Liverpool badala ya Manchester City, licha ya kuwa tayari yupo katika harakati za kufanya vipimo vya afya na matajiri hao wa jiji la Manchester.
Semenyo, mwenye umri wa miaka 26, anatarajiwa kujiunga na kikosi cha Pep Guardiola kwa ada ya Pauni 65 milioni ambayo iliwekwa kama bei katika mkataba wake kwa timu inayohitaji kuuvunja.
Mshambuliaji huyo ameng’ara sana akiwa na Bournemouth msimu huu, akifunga mabao 10 katika mechi 20, ikiwamo bao la ushindi dakika za majeruhi dhidi ya Tottenham Jumatano.
Licha ya ripoti nyingi kudai kuwa uhamisho wake kwenda Man City uko karibu kukamilika, kupitia Sky Sports Redknapp amesema: “Watu wengi wanaamini kila kitu kimekamilika, lakini mimi sina uhakika sana… nasikia Liverpool wameingia kwenye mchakato wa kutaka kumsajili.
“Nadhani Liverpool bado wapo kwenye harakati za kutaka kumsajili. Kwa kweli, nashangaa kwa nini hawajaingia kwa nguvu kama ilivyo kwa Man City, hasa ukiangalia nafasi ya Mohamed Salah, hatujui ataendelea kukaa katika timu kwa muda gani.
“Sisemi hii kama ni taarifa rasmi ya Sky Sports, lakini nilichosikia leo usiku ni kwamba huenda asiende Man City kama wengi wanavyodhani, mambo yanaweza kugeuko kidogo.:”
Akizungumza baada ya Semenyo kufunga bao la ushindi katika ushindi wa Bournemouth wa mabao 3-2 dhidi ya Spurs Jumatano, Iraola alimmiminia sifa nyingi mshambuliaji huyo.
“Si rahisi kufanya alichofanya. Wachezaji wengi wangetenda tofauti.
Hakuwahi kutafuta visingizio eti kwa sababu anahitajika na timu kubwa. Alikuwa tayari kutoa kile tulichohitaji.”
Kocha huyo pia alithibitisha kwamba Semenyo ataondoka na kinachosubiriwa ni taratibu za mwisho tu kukamilika.