Kombe la Dunia 2026: Marekani yajiandaa na tishio la magonjwa ya mlipuko
Muktasari:
- Wataalamu wa magonjwa ya kuambukiza katika majiji mbalimbali, ikiwemo New York, wako katika mafunzo makali ili kujiandaa na ongezeko la wageni ambalo linaweza kusababisha kuenea kwa magonjwa kwa kasi kubwa.
Serikali ya Marekani imeanza maandalizi makubwa ya kukabiliana na uwezekano wa kuingia kwa milipuko ya magonjwa hatari wakati wa michuano ya Kombe la Dunia 2026.
Wataalamu wa magonjwa ya kuambukiza katika majiji mbalimbali, ikiwemo New York, wako katika mafunzo makali ili kujiandaa na ongezeko la wageni ambalo linaweza kusababisha kuenea kwa magonjwa kwa kasi kubwa.
Inakadiriwa kuwa zaidi ya watu milioni 1.2 watatembelea majiji ya New York na New Jersey pekee, huku nchi nzima ikitarajia kupokea wageni zaidi ya milioni saba, jambo linalotajwa na madaktari kama tukio kubwa la uhamiaji.
Hofu kubwa imetanda miongoni mwa wataalamu wa afya kutokana na uwezekano wa wageni hao kubeba magonjwa yenye athari kubwa kama vile kifua kikuu, surua, malaria, homa ya matumbo, na hata virusi hatari vya Ebola.
Dokta Vikramjit Mukherjee, ambaye ni mkuu wa huduma za dharura katika Hospitali ya Bellevue, amesisitiza kuwa mfumo mzima wa afya utakuwa katika hali ya tahadhari.
Hospitali ya Bellevue ina uzoefu wa kipekee katika hili, kwani ndiyo iliyomtibu mgonjwa pekee wa Ebola jijini New York mwaka 2014, na hivyo wanahisi wana jukumu la ziada la kuwa mstari wa mbele kuzuia mlipuko mwingine wowote.
Katika kujiimarisha, majimbo ya New York na New Jersey yamekuwa yakifanya mazoezi ya dharura ya mara kwa mara, ikiwemo zoezi la siku nne la kusafirisha wagonjwa wa majaribio kwa njia ya anga kutoka Toronto hadi New York lililoshirikisha wahudumu 500.
Aidha, kipaumbele kikubwa kimewekwa katika kuhakikisha usalama wa wafanyakazi wa afya wanapoingia kwenye maeneo hatarishi. Sambamba na masuala ya afya, hospitali zimepewa maelekezo ya kuwa tayari kwa matukio ya dharura ya usalama kama vile mashambulizi ya risasi, ili kuhakikisha usalama wa jumla wa mashabiki na wakazi.
Ili kuratibu usalama huo kwa ngazi ya kitaifa, Idara ya Usalama wa Ndani ya Marekani imeunda kikosi kazi maalum cha FIFA kinachoongozwa na Andrew Giuliani. Kikosi hiki kimepewa dhamana ya kuhakikisha kuwa michuano hiyo, ambayo inatarajiwa kuwa mikubwa zaidi katika historia ya soka, inakuwa pia salama zaidi duniani.
Kwa kupitia mafunzo ya mfumo wa FEMA na ushirikiano wa karibu kati ya idara za afya na usalama, Marekani inalenga kudhibiti changamoto zote zinazoweza kujitokeza kutokana na muingiliano huo mkubwa wa mataifa.