Messi alivyotikisa MLS na kupita rekodi za Barcelona
Muktasari:
- Licha ya Miami kupoteza fainali ya U.S. Open 2023 na Kombe la Ligi 2025 pamoja na kutofika fainali ya Kombe la Shirikisho al Amerika Kaskazini (Concacaf), hakukuwa na upungufu mkubwa katika kiwango katika enzi ya Messi.
MIAMI, MAREKANI: WAKATI Lionel Messi aliposaini kuichezea Inter Miami majira ya kiangazi 2023, alibadilisha kabisa mwelekeo wa klabu hiyo na Ligi Kuu Marekani (MLS) kwa kiwango ambacho hakijawahi kushuhudiwa, isipokuwa tu kwa mmiliki mwenza wa klabu hiyo, David Beckham 2007.
Tangu hapo, Messi ameweka rekodia nyingi, ambapo katika mechi zake 100 za kwanza katika mashindano yote, amefunga mabao 86 na kutoa asisti 56.
Pia amekuwa mchezaji wa kwanza kushinda tuzo ya MVP ya MLS ya Landon Donovan mara mbili mfululizo na kushinda kiatu cha dhahabu cha ligi hiyo maarufu kama MLS Golden Boot 2025. Katika mechi hizo 100, nusu ya mabao hayo aliyafunga 2025 pekee, ambapo alipachika mabao 43 katika mechi 49 kwenye mashindano yote.
Hatua hii ni tofauti na katika safari yake ya kufikisha mechi 100 akiwa Barcelona, ambapo alifunga mabao 41. Ni kweli idadi hiyo ni ndogo ukilinganisha na aliyofunga akiwa Inter Miami, lakini ikumbukwe kwamba alikuwa na umri wa miaka 17 alipocheza mechi ya kwanza ya ushindani akiwa na klabu hiyo. Pia, alikumbana na ushindani mkali zaidi, lakini bado alikuwa na wastani wa karibu bao moja kila mechi 2.4.
Pia, mchezaji huyo amekuwa wa kwanza anayecheza MLS kushinda tuzo ya Ballon d’Or ikiwa ni ya nane kwake 2023, hasa kutokana na kiwango chake katika Kombe la Dunia 2022 akiwa na Argentina, ambapo walibeba ubingwa. Mbali na mafanikio yake binafsi akiwa na klabu hiyo ya Kusini mwa Florida, aliiongoza kushinda Kombe la Ligi 2023, Tuzo ya Mashabiki 2024 na MLS Cup 2025.
Hata hivyo, mara nyingi hajapenda kung’ara peke yake katika fainali, bali amekuwa akiwatengenezea nafasi wachezaji wenzake kuandika historia .
Licha ya Miami kupoteza fainali ya U.S. Open 2023 na Kombe la Ligi 2025 pamoja na kutofika fainali ya Kombe la Shirikisho al Amerika Kaskazini (Concacaf), hakukuwa na upungufu mkubwa katika kiwango katika enzi ya Messi.