Guardiola atuma meseji zito kwa mastaa wake

Muktasari:

  • Man City inafukuzia rekodi ya kunyakua taji la Ligi Kuu England kwa mara ya nne mfululizo, kwa sasa imeachwa nyuma pointi moja na vinara Arsenal, lakini wenyewe bado wana mechi tatu za kucheza, huku wapinzani wao hao wanaonolewa na Mikel Arteta wamebakiza mechi mbili, ikiwamo moja dhidi ya Manchester United itakayopigwa Jumapili hii.

MANCHESTER, ENGLAND: PEP Guardiola amewaambia wachezaji wake wa Manchester City  kosa moja tu litawafanya watoe mkono wa kwa heri kwa ubingwa wa Ligi Kuu England msimu huu.

Man City inafukuzia rekodi ya kunyakua taji la Ligi Kuu England kwa mara ya nne mfululizo, kwa sasa imeachwa nyuma pointi moja na vinara Arsenal, lakini wenyewe bado wana mechi tatu za kucheza, huku wapinzani wao hao wanaonolewa na Mikel Arteta wamebakiza mechi mbili, ikiwamo moja dhidi ya Manchester United itakayopigwa Jumapili hii.

Man City inaweza kushuka usukani wa ligi na kuipa presha Arsenal endapo kama itapata ushindi dhidi ya Fulha, Jumamosi kabla ya saa 24 baadaye, Arsenal haijaenda kwenye jambo lake huko Old Trafford.

Lakini, Guardiola alisema kucheza kabla au baada ya mechi ya Arsenal haileti tofauti yoyote, ambapo kocha huyo wa Etihad alisema wanachopaswa kufanya ni kushinda mechi zao zote.

“Kama tutacheza na Fulham kabla au baada ya mechi ya Arsenal, bado tunachohitaji ni ushindi,” alisema Guardiola na kuongeza. “Na Arsenal wanafahamu wazi wanapaswa kushinda.

“Si tu kwa wachezaji, bali kwa wafanyakazi wote pamoja na mashabiki, kila mmoja afahamu hatupaswi kufanya makosa, kwa sababu tunapoteza ubingwa wa Ligi Kuu England.

“Wanafahamu hilo, tunafahamu hilo, kwa kile kilichowatokea Liverpool siku chache zilizopita, niliwaambia wachezaji, tusiposhinda, basi tuseme kwaheri ubingwa, tutaonana msimu ujao.

“Hakuna utata. Tunaamini tutashinda dhidi ya Fulham, kisha Arsenal itakuwa na mechi Old Trafford, ambako Man United inapambania nafasi ya kucheza Europa League.”