Erling Haaland atishiwa kuuawa
Muktasari:
- Haaland ambaye alifunga bao la sita katika mechi tano za Ligi Kuu England msimu huu, hakuweza kuisaidia timu yake kupata ushindi dhidi ya Arsenal.
MANCHESTER, ENGLAND: MSHAMBULIAJI wa Manchester City, Erling Haaland amedai kupokea vitisho vya kuuawa baada ya kufunga bao katika sare ya 1-1 dhidi ya Arsenal.
Haaland ambaye alifunga bao la sita katika mechi tano za Ligi Kuu England msimu huu, hakuweza kuisaidia timu yake kupata ushindi dhidi ya Arsenal.
Baada ya mechi alionekana akisogea kwa mashabiki ambapo mmoja kati yao alimpa jezi aliyokuwa amevaa kisha akaingia katika vyumba vya kubadilishia nguo.
Alipoingia katika gari akiwa anaondoka aliweka picha katika mtandao wa Snapchat iliyoonyesha mashabiki wachache wa Arsenal wakiwazomea wachezaji wa Man City wakati basi lilipokuwa linatoka kwenye Uwanja wa Emirates.
Haaland akaposti tena katika mtandao wa Snapchat, ambapo aliweka picha yake kisha akaweka na ujumbe wa vitisho vya kuuliwa aliotumiwa kisha akaandika:”Pia sasa napokea vitisho vya kuuliwa.”
Kwenye picha hiyo kulikuwa na ujumbe kutoka kwenye akaunti ya Snapchat yenye jina Dara uliosomeka: “Angalia kwa makini sasa rafiki. Usijaribu kuchapisha kitu kingine kwenye Snapchat au itakuwa ndio mwisho wako.”