Ghana yaibana England, Partey arejea kikosini
Muktasari:
- Ghana ilikubali kuwa timu ya pili mbele ya England, ikitumia muda mwingi wa mchezo huo kuwa nyuma ya mpira na kuwaacha wenzao wakitawala.
Ghana imefanikiwa kusimamia mpango wake wa kujilinda, ikiibana England na kugawana pointi kwenye mchezo wa pili wa hatua ya makundi wa Fainali za Kombe la Dunia 2026.
Ghana ilikubali kuwa timu ya pili mbele ya England, ikitumia muda mwingi wa mchezo huo kuwa nyuma ya mpira na kuwaacha wenzao wakitawala.
England imeongoza kwa umiliki wa mpira vipindi vyote viwili lakini ikashindwa kutengeneza mashambulizi makubwa ya kuamua mchezo huo.
Hatua ya Ghana kucheza kwa kujilinda, kuliifanya England kusubiri mpaka dakika ya 57 kupata shuti lao la kwanza lililolenga lango kupitia kiungo Declan Rice.
Ndani ya dakika 90, England ikafanikiwa kupiga mashuti matatu pekee yaliyolenga lango huku Ghana ikipiga moja ikishambulia kwa kushtukiza.
Habari njema kwa Ghana ni kwamba kiungo wake Thomas Partey amecheza mechi yake ya kwanza kwa dakika zote tisini baada ya kuwa na ruhusa ya kuingia nchini Marekani.
Partey alikosekana mechi ya kwanza dhidi ya Panama baada ya Canada kumnyima visa ya kuingia nchini humo kutokana na madai ya kesi yake ya unyanyasi wa kingono na ubakaji ambapo mwenyewe ameyakanusha.
Matokeo hayo yanazifanya timu hizo kulingana pointi kwenye kundi L zote zikiwa na nne, huku England ikiwa juu ikifuatiwa na Ghana, kisha Panama na Croatia zikifuata chini zote zikiwa hazina pointi, zikitarajiwa kukutana baadaye leo.