DAH! Gyokeres shida bado iko palepale
Muktasari:
- Arsenal ilimtoa uwanjani straika huyo wakati wa mapumziko katika mchezo wa ushindi wa mabao 2-0 dhidi ya Burnley wikiendi iliyopita na alikosa pia mechi ya Ligi ya Mabingwa Ulaya, ambapo chama lake liliifanya kweli ugenini dhidi ya Slavia Prague, Jumanne iliyopita.
LONDON, ENGLAND: STRAIKA, Viktor Gyokeres amewekwa kando kwenye kikosi cha Sweden kitakachocheza mechi za kufuzu Kombe la Dunia dhidi ya Slovenia na Uswisi baadaye mwezi huu kutokana na kuwa majeruhi.
Arsenal ilimtoa uwanjani straika huyo wakati wa mapumziko katika mchezo wa ushindi wa mabao 2-0 dhidi ya Burnley wikiendi iliyopita na alikosa pia mechi ya Ligi ya Mabingwa Ulaya, ambapo chama lake liliifanya kweli ugenini dhidi ya Slavia Prague, Jumanne iliyopita.
Kiungo Mikel Merino alisogezwa mbele na kucheza kama straika, ambapo alifunga mara mbili katika ushindi wa 3-0 katika mechi hiyo. Na taarifa za karibuni kutoka Sweden ni kwamba Gyokeres haonekani kama atacheza dhidi ya Sunderland, Jumamosi. Sweden inayonolewa na aliyekuwa kocha wa Chelsea, Graham Potter, alimjumuisha Alexander Isak kwenye kikosi, lakini hakukuwa na nafasi kwa Gyokeres.
Taarifa ya chama cha soka cha Sweden iliyowekwa kwenye tovuti yake ilibainisha kwamba Gyokeres na staa wa Tottenham, Dejan Kulusevski wamekosekana kutokana na kuwa majeruhi.
Kocha wa Arsenal, Mikel Arteta alijadili kuhusu hali ya Gyokeres kwenye mkutano wa waandishi wa habari wa Jumatatu siku moja kabla ya timu yake haijakipiga kwenye Ligi ya Mabingwa.
“Hatakuwapo,” amesema Arteta akimzungumzia straika huyo wa zamani wa Sporting Lisbon.