Chelsea yampa Alonso miaka minne
Muktasari:
- Ripoti zinaeleza kuwa Chelsea imempa Alonso mamlaka makubwa zaidi kwenye usajili pamoja na fedha za kutosha kusajili nyota wakubwa dirisha lijalo.
LONDON, ENGLAND: KLABU ya Chelsea imethibitisha rasmi kumteua Xabi Alonso kuwa kocha mpya wa klabu hiyo kwa mkataba wa miaka minne.
Alonso, ambaye aliwahi kuinoa Real Madrid, anatarajiwa kupewa jukumu la kuirejesha Chelsea kwenye ubora wa soka la Ulaya baada ya kupotea kwa miaka ya hivi karibuni.
Ripoti zinaeleza kuwa Chelsea imempa Alonso mamlaka makubwa zaidi kwenye usajili pamoja na fedha za kutosha kusajili nyota wakubwa dirisha lijalo.
Tofauti na makocha waliopita, Alonso amepewa hadhi ya meneja badala ya kocha mkuu jambo linalomaanisha atakuwa na sauti kubwa kwenye maamuzi ya klabu.
Anakuwa kocha wa sita wa kudumu chini ya umiliki wa Todd Boehly na Behdad Eghbali baada ya Thomas Tuchel, Graham Potter, Mauricio Pochettino, Enzo Maresca na Liam Rosenior.
Viongozi wa Chelsea wamekubali kuwa timu imepoteza mwelekeo msimu huu baada ya kushindwa kufikia viwango vilivyotarajiwa, huku nafasi ya kushiriki michuano ya Ulaya msimu ujao ikiwa shakani.
Alonso anatarajiwa kufanya kazi kwa karibu na wakurugenzi wa michezo wa klabu hiyo, wakiongozwa na Paul Winstanley pamoja na Laurence Stewart, lakini safari hii akiwa na ushawishi mkubwa zaidi kwenye usajili na maamuzi ya timu.