Bosi Mamelodi awaza kupenya kundi gumu

Muktasari:
- Mabingwa hao wa Afrika Kusini walitarajia kukipiga na Ulsan Hyundai ya Asia katika mchezo wa kwanza wa hatua ya makundi ya fainali hizo za Marekani, usiku wa Jumanne kwenye Uwanja wa Inter Miami.
MIAMI, MAREKANI: KOCHA wa Mamelodi Sundowns, Miguel Cardoso amesema itakuwa mafanikio makubwa kwa timu yake endapo itapenya kwenye Kundi F, alilolitaja kuwa ni la kifo katika fainali za Kombe la Dunia la Klabu huko Marekani.
Mabingwa hao wa Afrika Kusini walitarajia kukipiga na Ulsan Hyundai ya Asia katika mchezo wa kwanza wa hatua ya makundi ya fainali hizo za Marekani, usiku wa Jumanne kwenye Uwanja wa Inter Miami.
Kwenye kundi lake, Mamelodi itakipiga pia na miamba ya Ujerumani, Borussia Dortmund na mabingwa wa Copa Libertadores, Fluminense - huku mashabiki wengi wakiamini hilo ndilo kundi gumu zaidi kwenye fainali hizo.
“Ni lazima tukusanye pointi kwanza na hili linahitaji kiwango cha hali ya juu kwenye mechi,” alisema Cardoso.
“Nafahamu ushindani utakuwa mgumu sana, lakini bado tuna uzoefu wa kutosha. Ni lazima tupambane hadi mwisho ili kufikia na kuzidi matarajio ya michuano hii.”
Sundowns ilikamatia tiketi ya kucheza michuano hiyo baada ya kufanya vizuri kwenye mikikimikiki ya CAF kwa kipindi cha misimu minne iliyopita, ambapo mwezi uliopita ilicheza fainali ya Ligi ya Mabingwa Afrika na kupoteza mbele ya Pyramids FC.
Kocha Cardoso, 53, ambaye aliwahi kuinoa Esperance ya Tunisia anaamini ukubwa wa michuano hiyo utawapa wachezaji wake mzuka wa kufanya vizuri.