Ayari aiadhibu nchi ya baba yake, Sweden ikitamba Kombe la Dunia
Muktasari:
- Ayari, ambaye kabla ya kuchagua kuitumikia Sweden alikuwa na nafasi ya kuichezea Tunisia, alianza kucheka na nyavu mapema tu katika dakika ya saba kwa mkwaju ambao ulililoizamisha timu ya baba yake na kuiweka Sweden mbele.
KIUNGO Yasin Ayari amekuwa gumzo baada ya kufunga mabao mawili dhidi ya Tunisia, taifa ambalo angeweza pia kulitumikia kutokana na asili ya baba yake, huku Sweden ikiichapa timu hiyo mabao 5-1 katika mchezo wa Kundi F uliochezwa alfajiri ya leo, Jumatatu kwenye Uwanja wa Estadio Monterrey, Mexico.
Ayari, ambaye kabla ya kuchagua kuitumikia Sweden alikuwa na nafasi ya kuichezea Tunisia, alianza kucheka na nyavu mapema tu katika dakika ya saba kwa mkwaju ambao ulililoizamisha timu ya baba yake na kuiweka Sweden mbele.
Mchezo huo uliendelea kuwa wa kasi huku mshambuliaji nyota Alexander Isak akiongeza bao la pili dakika ya 30 baada ya kupokea pasi kutoka kwa Viktor Gyokeres.
Tunisia ilirejea mchezoni dakika ya 43 kupitia beki Omar Rekik aliyefunga kwa msaada wa Hannibal Mejbri na kuifanya timu yake kwenda mapumzikoni ikiwa nyuma kwa mabao 2-1.
Hata hivyo kipindi cha pili Sweden walikuwa bora zaidi kufuatia Gyokeres kupachuka bao la tatu dakika ya 59 baada ya kutengenezewa nafasi na Isak, kabla ya Mattias Svanberg kuongeza la nne dakika ya 84 katika bao lililohitaji uhakiki wa VAR.
Tunisia ilijaribu kutafuta njia ya kurejea mchezoni lakini safu ya ushambuliaji ilishindwa kutumia nafasi chache ilizopata huku Sweden ikionekana kuwa makini zaidi mbele ya lango.
Dakika za nyongeza ndipo Ayari alipohitimisha siku yake ya kihistoria kwa kufunga bao la tano na la pili, akipiga shuti kutoka nje kidogo ya eneo la hatari lililoenda moja kwa moja kwenye lango la Tunisia.
Bao hilo liliwafanya mashabiki wa Sweden kushangilia kwa furaha kubwa huku Ayari akithibitisha kuwa mmoja wa nyota walioanza vizuri zaidi fainali za Kombe la Dunia mwaka huu.
Ushindi huo mkubwa umeiweka Sweden katika nafasi nzuri ya kusaka tiketi ya hatua ya mtoano kwenye kundi lenye ushindani mkubwa linalojumuisha pia Japan na Uholanzi ambazo zilitoka sare ya mabao 2-2 katika mchezo wao wa kwanza.
Kwa Tunisia, kipigo hicho kimeongeza presha kuelekea mechi zijazo huku ikihitaji matokeo mazuri dhidi ya Japan na Uholanzi ili kuendelea kuwa na matumaini ya kusonga mbele.