Arteta ajiweka mtegoni England

Muktasari:

  • Arsenal inakwenda jino kwa jino na Manchester City kwenye mbio za kufukuzia ubingwa na kinachoonekana vita itakwenda hadi mwisho wa msimu.

LONDON, ENGLAND: Kocha wa Arsenal, Mikel Arteta huenda akakosa mchezo wa mwisho wa Ligi Kuu England dhidi ya Everton.

Arsenal inakwenda jino kwa jino na Manchester City kwenye mbio za kufukuzia ubingwa na kinachoonekana vita itakwenda hadi mwisho wa msimu.

Arsenal ipo kileleni kwa tofauti ya pointi moja dhidi ya Man City iliyopo kwenye nafasi ya pili, lakini yenyewe imecheza mechi moja zaidi, hivyo kupata ubingwa wanaomba wapinzani wao wateleze kwenye mechi tatu walizobakiza.

Kocha Arteta ni muhimu kweli kuwapo kwenye benchi la ufundi hasa kama wanataka kufanya vizuri kwenye mechi zao mbili zilizobaki kwenye msako huo wa ubingwa. Arsenal itasafiri kwenda kucheza na Manchester United, Jumapili hii huko Old Trafford, kabla ya kuwakabili Everton uwanjani Emirates.

Hata hivyo, Arsenal inaweza kumkosa Arteta kwenye benchi lake katika mechi ya mwisho ya msimu dhidi ya Everton kama atakosa nidhamu kwenye mechi ya Man United na kuonyeshwa kadi ya njano.

Mhispaniola huyo ameshaonyeshwa kadi tano za njano, hivyo kama ataonyeshwa moja zaidi, basi atalazimika kuwa nje ya uwanja kwa mchezo mmoja.

Arteta aliwahi kukosa mechi moja kutokana na adhabu hiyo, ambapo alikosa katika mchezo wa kichapo cha bao 1-0 kutoka kwa Aston Villa, Desemba mwaka jana. Makocha wa Ligi Kuu England wanaadhibiwa kila wanapoonyeshwa kadi tatu za njano na Arteta, ameonekana kuwa ni mkosefu wa nidhamu kwa kiasi kikubwa msimu huu, ambapo hadi sasa ameshaonyeshwa kadi tano za njano.

Alionyeshwa kadi za njano kwenye mechi dhidi ya Fulham, Luton na Brighton, na kwenye mechi zote mbili alizocheza dhidi ya Chelsea. Hivyo, kwenye mchezo wa Man United uwanjani Old Trafford anapaswa kuwa mtulivu kwa kuwa akionyeshwa kadi ya njano, itamgharimu kwenye mechi ya mwisho.