Amad awa shujaa Ivory Coast ikiichapa Ecuador
Muktasari:
- Ushindi huo umevunja rekodi ya Ecuador ya kutopoteza mechi 19 mfululizo na kuipa Ivory Coast pointi tatu muhimu kabla ya kukutana na Ujerumani katika mchezo wao unaofuata.
PHILADELPHIA, MAREKANI: NYOTA wa Manchester United, Amad Diallo, amekuwa shujaa wa Ivory Coast baada ya kufunga bao la ushindi dakika ya 90 na kuiwezesha timu hiyo kuanza vizuri fainali za Kombe la Dunia 2026 kwa kuichapa Ecuador bao 1-0 katika mchezo wa Kundi E uliochezwa usiku wa kuamkia leo, Jumatatu.
Ushindi huo umevunja rekodi ya Ecuador ya kutopoteza mechi 19 mfululizo na kuipa Ivory Coast pointi tatu muhimu kabla ya kukutana na Ujerumani katika mchezo wao unaofuata.
Ivory Coast iliingia kwenye mchezo huo ikiwa na morali kubwa baada ya kuifunga Ufaransa katika mchezo wa kirafiki mapema mwezi huu lakini ilikabiliwa na upinzani mkali kutoka kwa Ecuador.
Katika kipindi cha kwanza timu zote zilipata nafasi kadhaa za kufunga. Bazoumana Toure alikuwa wa kwanza kujaribu bahati yake kwa Ivory Coast lakini shuti lake lilizuiwa na kipa Hernan Galindez.
Ecuador ilijibu kwa mashambulizi ya nguvu yaliyokaribia kuzaa matunda, John Yeboah aliisumbua safu ya ulinzi ya Ivory Coast baada ya kutumia makosa ya Emmanuel Agbadou na kupiga shuti kali lililogonga mwamba wa juu.
Dakika chache baadaye Alan Minda naye alikaribia kuifungia Ecuador baada ya kupokea pasi nzuri kutoka kwa Pedro Vite, lakini juhudi zake ziligonga mwamba huo huo na kuwaacha mashabiki wa Amerika Kusini wakishika vichwa.
Baada ya mapumziko, Ivory Coast iliongeza kasi ya mashambulizi huku Yan Diomande akiwa mwiba mkubwa kwa mabeki wa Ecuador.
Mshambuliaji Elye Wahi alidhani ameifungia timu yake bao la kuongoza, lakini shuti lake la kwanza liligonga mwamba na kutoka.
Wakati wengi wakiamini mchezo huo ungeisha kwa sare tasa, Ivory Coast ilipata nafasi ya mwisho iliyoamua matokeo.
Dakika ya 90, beki Wilfried Singo alianza mbio kutoka eneo lake la ulinzi na kuvuka mabeki kadhaa wa Ecuador kabla ya kuingia ndani ya eneo la hatari.
Alipeleka pasi safi kwa Amad Diallo ambaye hakufanya makosa, akimalizia kwa utulivu na kumshinda Galindez.
Bao hilo liliwaamsha mashabiki wa Ivory Coast waliokuwa uwanjani na kusababisha shangwe huku wachezaji wa Ecuador wakibaki wamesimama kwa mshangao.
Mbali na ushindi huo, Ivory Coast ilipata habari njema baada ya kiungo mshambuliaji Yan Diomande kutangazwa kuwa mchezaji bora wa mechi kutokana na kiwango chake bora katika dakika zote 90.
Sasa Ivory Coast itajiandaa kwa mtihani mgumu dhidi ya Ujerumani katika mechi ijayo ya Kundi E huku Ecuador ikilazimika kutafuta ushindi dhidi ya Curaçao ili kujiweka katika nafasi nzuri ya kufuzu hatua ya mtoano.
Matokeo hayo yanaifanya Ivory Coast kuanza kwa kishindo safari ya kutafuta mafanikio makubwa katika Kombe la Dunia 2026 huku Ecuador ikipata pigo la kwanza baada ya karibu miaka miwili bila kupoteza mchezo wowote wa kimataifa.