Afrika Kusini yaitaka WAFCON 2026
Muktasari:
- Kwa mujibu wa waziri huyo, serikali ya Afrika Kusini iko tayari kuchukua jukumu la kuandaa mashindano hayo yatakayofanyika kuanzia Machi 17 hadi Aprili 3, 2026.
AFRIKA Kusini inatajwa kuwa kwenye nafasi nzuri ya kuwa mwenyeji wa michuano ya Kombe la Mataifa ya Afrika kwa Wanawake 2026 (WAFCON), kufuatia kauli ya Naibu Waziri wa Michezo wa nchi hiyo, Peace Mabe.
Kwa mujibu wa waziri huyo, serikali ya Afrika Kusini iko tayari kuchukua jukumu la kuandaa mashindano hayo yatakayofanyika kuanzia Machi 17 hadi Aprili 3, 2026.
Hata hivyo, taarifa hiyo imezua sintofahamu mitandaoni kwani awali Shirikisho la Mpira wa Miguu Afrika (CAF) liliipatia Morocco haki ya kuandaa mashindano hayo, hata droo ya hatua ya makundi tayari ilishafanyika Januari 2026, huku timu zikipangwa katika makundi manne tofauti.
Kuna sababu mbalimbali zinazotajwa kuwa Morocco wamesusa baada ya kulikosa Kombe la Mataifa ya Afrika kwa wanaume (AFCON) lililoenda kwa Senegal.
Licha ya madai hayo kutoka Afrika Kusini, CAF hadi sasa bado haijatoa tamko rasmi linalothibitisha mabadiliko ya nchi mwenyeji.
Morocco pia haijatangaza rasmi kujiondoa katika maandalizi ya mashindano hayo, na Shirikisho la Mpira wa Miguu la Morocco bado halijatoa taarifa yoyote kuhusu kuachia haki za uenyeji.
Iwapo Afrika Kusini itapewa ruhusa ya kuwa mwenyeji, itakuwa sio mara ya kwanza kwani taifa hilo liliwahi kuandaa WAFCON mwaka 2000, 2004 na mara ya mwisho mwaka 2010.
Tanzania kwenye mashindano hayo imepangwa kundi B na Afrika Kusini, Ivory Coast na Burkina Faso, hii ikiwa mara ya tatu kwa Twiga Stars kucheza mashindano hayo baada ya 2010 na 2024 kuishia hatua ya makundi.