Yanga yafuata mido Ulaya, tajiri ajipanga kuvunja benki

Muktasari:

  • Ni kiungo ambaye ukihesabu timu alizocheza Ulaya inashtua kidogo lakini Mwanaspoti limejiridhisha kwamba kupitia Cedrick Kaze na wakala wake Yanga inapambana kumshawishi atue Tanzania.

YANGA imemalizana na Bernard Morrison akisaini mkataba wa mwaka mmoja kurejea klabuni kwa masharti kadhaa lakini kuna balaa kubwa wanalifanyia kazi kwa usiri mkubwa.

Yanga imeweka wazi kwamba wanashusha mastaa watano wa kigeni na jina kubwa jingine ni Mrundi Gael Bigirimana.

Ni kiungo ambaye ukihesabu timu alizocheza Ulaya inashtua kidogo lakini Mwanaspoti limejiridhisha kwamba kupitia Cedrick Kaze na wakala wake Yanga inapambana kumshawishi atue Tanzania.

Amepitia klabu kama Coventry City, Newcastle United, Rangers na sasa Glentoran ya Ireland ya Kaskazini. Matajiri wa Yanga, GSM wako katika mazungumzo ya kumrudisha Afrika, Bigirimana ambaye ni tegemeo kwenye timu ya Taifa ya Burundi amewahi kutamba na Newcastle United ya England ambayo anaishabikia Rais mstaafu Jakaya Kikwete.

Faili la usajili mpya wa kocha wa Yanga, Nasreddine Nabi linahitaji kupata kiungo aina ya Gael ambaye anayecheza staili ya ‘box to box’.

Mwanaspoti linafahamu kwamba meneja wa mchezaji huyo ambaye anaishi nchini England anakaribia kukamilisha dili hilo ambalo litakuwa ni usajili wa mwisho kwa Yanga kwa wachezaji wa kigeni.

Ushawishi mkubwa ambao Yanga imeutumia kwa Bigirimana ni ofa kubwa ambayo wamempa kiungo huyo ambaye pia alikuwa na uhitaji wa kuja kukaa karibu na familia yake Burundi.

Bigirimana licha ya ofa ya Yanga bado alikuwa anashindwa kuwa na uhakika na maisha ya Ulaya kutokana na kiwango chake kuwekewa mashaka ambapo akiwa na Glentoran amecheza mechi 43 bila bao. Yanga wamekuwa wasiri zaidi kwenye usajili huo na wanataka kuufanya kama sapraizi.

Mpaka sasa Yanga imeshawasainisha mshambuliaji Mzambia Lazarous Kambole, Mghana Morrison ambao wameshawatambulisha huku beki wa kushoto Mkongomani Lucy Lomalisa, Aziz KI na Bigirimana wakiwa bado hawajambulishwa.


MORRISON

Habari za uhakika ambazo Mwanaspoti inazo ni kwamba Morrison ambaye tulikuwa wa kwanza kukupata habari za usajili wake, amesajiliwa Yanga kwa masharti mazito haswa ya nidhamu. Habari zinasema kwamba ameambiwa ajirekebishe kwa kiasi kikubwa na kuacha vitendo vya utovu wa nidhamu ambavyo havina manufaa kwa timu. Lakini ametakiwa kufanya mazoezi kwa nguvu pamona kuipambania timu ndani ya dakika zote bila kuchagua mechi. Tayari ameshapewa programu.