Yanga wampa saluti Hersi

WANACHAMA wa Yanga wamempa sifa mjumbe wa Kamati ya Usajili ya Yanga, Hersi Said kwa kufanikisha usajili bora wa msimu huu.

Hayo yamesemwa na wanachama wa timu hiyo tawi la Yanga Mashujaa lililopo Kiwalani Kigilagila, Dar es Salaam baada ya kuona chama lao likianza vyema msimu huu kwa kushinda michezo yote miwili ya Ligi Kuu Bara iliyocheza wakiifunga Geita Gold kwa bao 1-0 na kushinda ugenini 1-0 dhidi ya Kagera Sugar.

Katibu wa tawi hilo, Ramadhan Mwinyimkuu alisema kuwa Hersi anapaswa kupewa pongezi kwa usajili alioufanya msimu huu kwani ni ishara tosha wamejifuza kutokana na makosa waliyofanya misimu iliyopita.

“Katika kipindi cha miaka minne huu nadhani ni usajili bora, ingawa bado ni mapema ila unaona kabisa wachezaji wanacheza vizuri kitu ambacho tulikuwa tunakikosa,” alisema.

Mweny

ekiti wa tawi, George Shaban alisema kwa wachezaji waliosajiliwa ni suala la muda tu kwani wakikaa pamoja muda mrefu na kuelewana itakuwa bonge la timu ambayo itasumbua zaidi ya misimu minne waliyokosa ubingwa.


“Tunapaswa kumuunga mkono kocha wetu hatuna kisingizio kuhusu timu tena. Tumeona wachezaji ni wazuri wanapaswa kupata michezo mingi ili kutengeneza muunganiko,” alisema.

Mjumbe wa tawi hilo, Raphael Ganila, alisema kazi iliyobaki kwa kocha ni kuongeza uimara kwa wachezaji kwani wanaanza vizuri ila wanachoka haraka.

“Kipindi cha kwanza unaona timu inapambana sana lakini cha pili inakata moto. Nabi alizingatie sana hilo kwa kuwapa mechi nyingi katika kipindi hiki cha michezo ya kimataifa,” alisema.


DIARRA, BANGALA NA AUCHO

Ismail Ally ambaye ni mjumbe wa tawi, alisema licha ya ubora wa wachezaji kwenye kikosi chao anaamini kipa Djigui Diarra na viungo Yannick Bangala na Khalid Aucho watakuwa chachu yao kutimiza malengo ya kutwaa ubingwa msimu huu.

“Timu inatengenezwa kuanzia nyuma kwenda mbele na hilo tumeliona. Ubora wa wachezaji wetu walionao hususani kwenye kukaa na mpira kunaonyesha mwanga kwenye kikosi, jambo ambalo hapo mwanzo halikuwepo,” alisema.

Tawi hilo lenye wanachama 86 lilianzishwa 2016 likiongozwa na Mwenyekiti Junedi Mustapha na msaidizi wake, Miraji Miraji, Ramadhan Mwinyimkuu (katibu mkuu) akiwa na msaidizi wake Amri Juma pamoja na Mtunza Fedha, Selemani Hamisi.