Waziri Jr atumia dakika 10 kuipa furaha Yanga

USIKU wa jana inawezekana ukawa ni usiku mkubwa kwa wapenzi wa klabu ya Yanga baada ya kuwa na mchezo mgumu wa Ligi Kuu dhidi ya Mwadui ukimalizika wakishinda 3-2.

Mshambuliaji wa Yanga, Wazir Junior aliingia dakika 81 akichukua nafasi ya Saido Ntibazonkinza na alifunga bao la tatu na ushindi na kuwafanya mashabiki watoke kifua mbele katika uwanja wa Benjamin Mkapa baada ya kuwa muda wote kuwa katika presha.

Junior alifunga bao hilo dakika 92 akiunganisha pasi ya Tuisila Kisinda aliyopiga krosi ya chini chini na mshambuliaji huyo alionganisha na mpira ukaenda wavuni.

Hilo linakuwa ni bao la pili kwa Junior msimu huu akiwa na klabu ya Yanga aliyojiunga nayo akitokea Mbao FC ambayo imeshuka daraja msimu uliopita.

Junior msimu uliopita alikuwa kwenye kiwango kikubwa baada ya kupata nafasi ya kucheza na aliifungia Mbao mabao 13 huku akiwa mchezaji bora wa msimu mara mbili mfululizo.

Katika mchezo huo Yanga walikuwa katika wakati mgumu kwa dakika zote, huku bao la kwanza likifungwa dakika ya saba tu na Aniceth Revocatus mshambuliaji huyu alifunga mara mbili.

Upande wa Yanga mabao yao yalifungwa na Bakari Mwamnyeto, Yacouba Songne na Wazir Junior.