Usalama waimarishwa Kwa Mkapa

Muktasari:

  • Kama Jeshi la Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam lilivyoahidi ulinzi kufanyika barabara zote zilizo karibu na Uwanja wa Mkapa, hilo limefanyika kwani wamejazwa kila kona.

LICHA ya uchache wa mashabiki kabla ya mchezo wa watani wa jadi, Yanga dhidi ya Simba unaotarajiwa kupigwa saa 11:00 jioni, usalama umeimarishwa kila kona.

Kama Jeshi la Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam lilivyoahidi ulinzi kufanyika barabara zote zilizo karibu na Uwanja wa Mkapa, hilo limefanyika kwani wamejazwa kila kona.

Ili kuhakikisha usalama unakuwepo polisi wamejipanga mageti yote ya kuingilia mashabiki kwa idadi kubwa, huku wakionekana kukagua mashabiki wachache waliojitokeza mapema kabla ya mchezo.

Kama ilivyozoeleka mashabiki kupanga mistari kwa ajili ya kuingia uwanjani, kwa leo hadi muda wa saa 6:30 mchana hakukuwa na foleni waliowahi wanaingia kwa ustaarabu bila fujo kutokana na kukosekana kwa msongamano wa watu.

Ukaguzi unafanyika kuanzia wanaoingia kwa miguu na wale wenye magari binafsi ambapo wanakaguliwa kwa lengo la kuhakikisha usalama zaidi.

Yanga itakuwa timu mwenyeji kwenye mchezo huo ambao ni wa mzunguko wa pili wa Ligi Kuu Bara, huku ikiingia ikiwa na kumbukumbu ya matokeo mazuri mchezo wa kwanza wakishinda mabao 5-1.