Tegete: Yanga wasajili nyota hawa

KOCHA mkongwe John Tegete amesema amekifuatilia kikosi cha Yanga na kugundua kuwa timu hiyo inahitaji kufanya usajili kwa umakini mkubwa wachezaji wanne wa kimataifa wenye viwango bora.

Tegete alisema nafasi ambazo ameona Yanga wanatakiwa kusajili ni kipa, beki wa kati na washambuliaji wawili wakali ambao kwake angetamani kuona wanatoka nje ya nchi na wawe wanacheza kwenye timu kubwa barani Afrika.

Alisema kama Yanga wakifanya usajili huo basi msimu ujao watakuwa na kikosi bora ambacho kitafanya vizuri msimu ujao wa Ligi Kuu na michuano ya kimataifa.

‘‘Kwangu naona Yanga wanahitaji kusajili nyota wanne tu kutoka timu kubwa Afrika na wawe na kiwango bora wakifanya hivyo basi msimu ujao naamini watanyakua ubingwa bila wasiwasi.

‘‘Yanga wanatakiwa kuwa makini sana kipindi hiki ambacho wanasajili wachezaji wasikurupuke kusajili mchezaji kwa presha ya timu nyingine bali wawe watulivu ili wapate nyota wazuri watakaosaidia timu,’’ alisema kocha huyo.

Hadi sasa Yanga wamefanya usajili wa beki wa kushoto, Shaban Djuma raia wa DR Congo, na wapo kwenye mazungumzo na Fiston Mayele wa AS Vita ya nchini humo.