Simba yatakata Kirumba, Kagere akiweka 2

Simba yatakata Kirumba, Kagere akiweka 2

MABAO matatu yaliyofungwa na Meddie Kagere na Kibu Denis yametosha kuifanya Simba iende mapumziko ikiwa mbele kwa mabao 3-0 dhidi ya Ruvu Shooting katika Uwanja wa CCM Kirumba Mwanza.

Simba wameuanza vizuri mchezo huo wakishambulia kwa kasi na kutandaza soka safi lililowapa burudani mashabiki waliokuwa wakilipuka kwa shangwe.

Dakika ya 17 Meddie Kagere aliiandikia timu yake bao la kwanza akiunganisha mpira wa kona uliopigwa na Bernad Morrison ikiwa ni baada ya kosa kosa langoni mwa Ruvu Shooting.

Meddie Kagere alirudi tena nyavuni akiiandikia Simba bao la pili mnamo dakika ya 36 akimalizia mpira uliotemwa na Kipa Mohamed Makaka akiokoa shuti la Kibu Denis aliyepokea pasi safi kutoka kwa Bernad Morrison.

Simba iliandika bao la tatu katika dakika ya 44 likifungwa na Kibu Denis akitumia vyema faida iliyotengenezwa na Meddie Kagere aliyemhadaa kipa na kukwepa krosi ya chini chini iliyochongwa na Shomari Kapombe.

Dakika ya 4 Bernad Morrison aliangushwa katika eneo la hatari lakini mwamuzi Ahmed Arajiga kutoka Manyara akapeta huku Uwanja ukilipuka kwa kelele kumlaumu refarii.

Tukio hilo lilisababisha Morrison kupewa kadi ya njano baada ya kumzonga mwamuzi.

Morrison aliendelea kuonekana nyota wa mchezo akionyesha ufundi wake ambapo dakika ya 31 Cassian Ponera alionyeshwa kadi ya njano ya kumshika Morrison aliyekuwa akijaribu kumtoka.

Mchezo huo utaendelea hivi punde baada ya mapumziko.