Simba yashusha kocha mpya

Simba yaleta kocha mpya

ACHANA na furaha waliyokuwa nayo Simba baada ya kufuzu kwa mara ya kwanza hatua ya makundi Kombe la Shirikisho Afrika, Uongozi wa timu hiyo umeendelea kulisuka benchi la ufundi.

Ili kuhakikisha wanakuwa na benchi la ufundi imara na kufuata matakwa ya kocha wao, Pablo Franco jana Jumatatu walimshusha nchini kocha mpya wa makipa.

Mwanaspoti lilimnasa kocha huyo, Msauzi Tyron Damons (43), aliyetua nchini akiwa na wakala wake kisha kupokelewa na Simba na kwenda kufichwa katika hoteli moja jijini Dar es Salaam.

Damons baada ya kutua nchini sambamba na wakala wake wanamsubiri, Ofisa Mtendaji mkuu wa Simba, Barbara Gonzalez pamoja na Mwenyekiti wa bodi, Salim Abdallah ‘Try Again’ waliopo Zambia.

Baada ya viongozi hao wawili wakubwa ngazi ya juu Simba kufika nchini leo watakutana na Damons kisha kujadiliana juu ya mkataba na baada ya hapo atasaini.

Damons baada ya kusaini mkataba huo atapelekwa kambini kutambulishwa kwa benchi la ufundi pamoja na wachezaji na ataanza kazi ya kuwanoa makipa, Aishi Manula, Ally Salim, Benno Kakolanya na Jeremia Kisubi kama ambavyo ratiba yao itaeleza.

Kibarua cha kwanza kwa Damons itakuwa mechi kubwa ya dabi Simba na Yanga ambayo itakayochezwa Desemba 11, Uwanja wa Mkapa. Msauzi huyo amekuja nchini kuchukua nafasi ya kocha wa makipa, Mbrazil Milton Nienov ambaye mwezi uliopita alionyeshwa mlango wa kutokea muda mchache baada ya Simba kuondolewa kwenye michuano ya Ligi ya Mabingwa Afrika.Damons ametoka kufundisha timu ya TS Galaxy FC inayoshiriki Ligi Kuu Afrika Kusini aliyojiunga nayo, Oktoba 18, 2020, kabla ya hapo alikuwa, Bidvest Wits ya nchini humo.

Damons kabla ya kuwa kocha wa makipa, alikuwa mchezaji na alipita timu za Royal AM Youth, Vasco Da Gama, Winners Park Fc, Mbabane Swallows, Dynamos Fc, na mwaka 2013 alistaafu kucheza soka la ushindani akiwa na kikosi cha Bidvest Wits.