Simba, Yanga Zanzibar kesho ni shida!
Muktasari:
Simba, Yanga na Singida zitakazocheza kesho, zimeungana na Azam FC kukamilisha timu nne zinazotoka Tanzania Bara. Azam wao ndiyo walizifungulia dimba timu hizo za Bara walipocheza mchezo wao Jumapili iliyopita wakaifunga Mwenge mabao 2-0.
WAKONGWE wa Ligi Kuu Bara klabu za Simba na Yanga kesho Jumanne zitaanza kutupa
karata yao ya kwanza kwenye mashindano ya Kombe la Mapinduzi na mechi zote zitachezwa Uwanja wa Amaan, Kisiwani Zanzibar.
Simba ambayo ni vinara wa ligi kuu, watacheza mechi yao saa 10:30 jioni dhidi ya Mwenge ya Pemba na Yanga ambao wameondoka kwenye ligi ya Bara na kilio cha kufungwa mabao 2-0 na Mbao FC, wataingia uwanjani saa 02:15 usiku, kukipiga na Mlandege ya Zanzibar.
Hata hivyo, kesho hiyo ya Jumanne, klabu inayoshiriki mashindano hayo kwa mara ya Singida United, itakipiga na Zimamoto mchana wa saa 08:30.
Simba, Yanga na Singida zitakazocheza kesho, zimeungana na Azam FC kukamilisha timu nne zinazotoka Tanzania Bara. Azam wao ndiyo walizifungulia dimba timu hizo za Bara walipocheza mchezo wao Jumapili iliyopita wakaifunga Mwenge mabao 2-0.
Simba imepangwa kundi A pamoja na timu za Azam, Jamhuri, Zimamoto na Mwenge za Zanzibar pamoja na URA ya Uganda, Yanga ipo kundi A na timu za Singida united, pamoja na Mlandege, JKU na Taifa ya Jan’gombe za Zanzibar.