Simba, Yanga mbona fresh tu

Unguja. Ni tofauti kabisa na namna inavyokuwa kwenye viwanja vya soka Bara ambapo mashabiki wa Simba na Yanga hawawezi kukaa pamoja lakini kisiwani hapa maisha ni tofauti kabisa.

Leo Jumatano katika fainali ya Kombe la Mapinduzi ambayo inazikutanisha Simba na Yanga zote kutoka Bara na ni watani wa jadi mashabiki wao wamekaa pamoja na wanacheza muziki kwa pamoja.

Muziki unaopigwa uwanjani hapa ni kutoka kwa wasanii mbalimbali ulimwenguni ambao unapigwa na waandaaji wa mashindano hayo hivyo kuwafanya mashabiki hao kucheza kwa pamoja huku wakitaniana.

Simba na Yanga zikicheza mechi yoyote huko Bara hata kama hawakutani wenyewe kwa wenyewe basi hakuna shabiki atakayekwenda kwenye jukwaaa la mwenzake na ikitokea hivyo basi shabiki huyo lazima atakutana na gharika ya kipigo ama vurugu yoyote ile ya kumkera mpaka anaondoka.

Mechi ya fainali hiyo inatarajiwa kuanza kuchezwa saa 2 usiku ambapo baadaye kutakuwepo na burudani kutoka kwa wasanii Harmonize na Nandy huku mgeni rasmi ni Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Wawakilishi, Dr Hussein Mwinyi.