Simba yaingia saiti Zenji

Simba yaingia saiti Zenji

Muktasari:

  • KIKOSI cha Simba kimeondoka  leo, Ijumaa  jijini Dar es Salaam kwenda Zanzibar ambako kitaweka kambi ya wiki moja kufuatia kusimama kwa mikiki ya Ligi Kuu Bara.

KIKOSI cha Simba kimeondoka  leo, Ijumaa  jijini Dar es Salaam kwenda Zanzibar ambako kitaweka kambi ya wiki moja kufuatia kusimama kwa mikiki ya Ligi Kuu Bara.

Awamu iliyopita kikosi hicho ambacho kwa sasa kinanolewa na Juma Mgunda, kikiwa na Mserbia, Zoran Maki kabla ya kuachana na timu hiyo,  kilienda Sudan.

Kikosi hicho ambacho kilikuwa na wachezaji ambao hawakuitwa kwenye timu zao za taifa kipindi hiki cha wiki ya kimataifa kiliwasili bandarini saa nane mchana tayari kwa safari hiyo.

Mashabiki wa timu hiyo nao hawakuwa nyuma, walijitokeza kuwaaga nyota wao ambao msimu huu wanajukumu la kurejesha mataji yao ambayo msimu uliopita watani zao waliyatwaa.

Wapo ambao walikuwa wakipigana vikumbo kutaka kupiga picha na nyota hao ambao kwenye michezo minne ya Ligi Kuu Bara, wameifanya Simba kuvuna pointi 10 ambazo zimewafanya kuwa nafasi ya pili nyuma ya Yanga huku wakipishana kwa mabao ya kufunga na kufungwa.

Baadhi ya wachezaji ambao walionekana kwenye msafara huo ni pamoja na nahodha, John Bocco, Kennedy Juma, Peter Banda, Nassor Kapama, Dejan Georgijevic na Moses Phiri ambaye anaonekana kuwa kwenye kiwango bora tangu ajiunge na wekundu hao wa Msimbazi.

Wengine ni Israel Mwenda, Kibu Dennis, Victor Akpan, Nelson Okwa, Gadiel Michael, Sadio Kanoute, Jymson Mwanuke, Mzamiru Yassin.