Ripoti ya Singida Black Stars inataka sita wapya
Muktasari:
- Singida Black Stars imemaliza Ligi Kuu msimu wa 2025-2026 katika nafasi ya nne ikikusanya pointi 50 na kujihakikishia kushiriki michuano ya Kombe la Shirikisho Afrika ikiwa ni msimu wa pili mfululizo ikifanya hivyo na msimu uliopita iliishia hatua ya makundi.
WAKATI uongozi wa Singida Black Stars ukitarajia kupokea ripoti ya benchi la ufundi, kocha wa timu hiyo, Muhibu Kanu amesema anajivunia kutimiza malengo ya kumaliza nafasi ya nne kwenye msimamo wa Ligi Kuu ya NBC, akifichua kilichomo kwenye ripoti anayoiwasilisha.
Singida Black Stars imemaliza Ligi Kuu msimu wa 2025-2026 katika nafasi ya nne ikikusanya pointi 50 na kujihakikishia kushiriki michuano ya Kombe la Shirikisho Afrika ikiwa ni msimu wa pili mfululizo ikifanya hivyo na msimu uliopita iliishia hatua ya makundi.
Akizungumza na Mwanaspoti, Kanu amesema licha ya kukabidhiwa majukumu kipindi kigumu, lakini anajivunia kufikia malengo aliyopewa na kwamba anapoenda kukabidhi ripoti ameainisha kila kitu kwa mustakabali wa msimu ujao.
Amesema kwakuwa Singida inajiandaa na mashindano mengi ya ndani na nje, anahitaji kuwa na kikosi bora na imara ambacho kitahimili michezo yote na kulinda hadhi na heshima ya klabu.
“Kwa maana hiyo katika ripoti nimetaja kuhitaji wachezaji sita ikiwamo wanne wa kigeni na wawili wa ndani, hivyo kuna ambao wataondoka kupisha sura hizo na tumetaja majina ya tunaowataka na nafasi zao kikosini.
Kocha huyo ameongeza, kutokana na ratiba waliyonayo msimu ujao, hawatakuwa na muda mwingi wa kupoteza kukaa likizo, badala yake wanatarajia kuanza mapema kambi kujiandaa ikiwamo kucheza mechi za kirafiki.
Baada ya kukabidhiwa mikoba, Kanu ameiongoza Singida katika mechi 12 akishinda nane, sare mbili na kupoteza mbili na kumaliza nafasi nne za juu na kuwa na uhakika wa kuwakilisha nchi kimataifa.