Rais Samia ampa zawadi ya fedha Changalawe na wenzake

Muktasari:

  • Mabondia waliofanya vizuri katika mashindano hayo mbali ya Changalawe ni Mussa Maregesi na Ezra Paul ambao walifanikiwa kupata medali za shaba huku zawadi hizo zikikabidhiwa na Katibu Mkuu wa Wizara ya Utamaduni, Sanaa na Michezo, Gerson Msigwa.

RAIS wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, amemzawadia zawadi ya fedha nahodha wa timu ya taifa ya Faru Weusi wa Ngorongoro, Yusuph Changalawe na wenzake kutokana na kufanikiwa kushinda medali tatu za shaba katika michuano ya All African Games.

Mabondia waliofanya vizuri katika mashindano hayo mbali ya Changalawe ni Mussa Maregesi na Ezra Paul ambao walifanikiwa kupata medali za shaba huku zawadi hizo zikikabidhiwa na Katibu Mkuu wa Wizara ya Utamaduni, Sanaa na Michezo, Gerson Msigwa.

Mbali na mabondia hao, pia makocha wao Samweli Kapungu na Muhsini Mohamed walipatiwa zawadi kutokana na kufanya vyema katika mashindano hayo na kuiletea heshima Taifa. Serikali imewapatia kiasi cha fedha kama chachu ya kuongeza bidii na pongezi kwao.

Msigwa alisema kuwa, Rais Dkt Samia amewazawadia mabondia hao kutokana na kufanya vizuri katika michuano hiyo iliyofanyika Accra nchini Ghana kuanzia Machi 8 hadi 23, 2024 kwa kuendelea kuipa heshima Tanzania kutokana na medali walizoshinda.