Ninja achekelea Mapinduzi kuwabeba mastaa wa Zanzibar

MICHUANO ya Kombe la Mapinduzi imemalizika jana Jumatano kwa kuzikutanisha Simba na Yanga kwenye fainali hizo zilizochezwa Uwanja wa Amaan, huku beki wa Yanga Abdallah Shaibu ‘Ninja’ akitamka neno.

Ninja alisema wachezaji wengi wa Zanzibar hutumia mashindano hayo kujitangaza kwa timu za Bara ambapo, hata yeye alitoonekana kwenye mashindano hayo mpaka Yanga wakamsajili na baadaye kutoboa hadi Marekani.

Beki huyo wa kati aliliambia Mwanaspoti kuwa, mara nyingi michuano imekuwa ikiwapa dili Wazenji na kudai ndio maana hata timu shiriki za Zanzibar zinapokutana na timu za Bara wachezaji hujituma zaidi tofauti na wanapokutana wao kwa wao.

“Kwa Zanzibar michuano hii ni mikubwa sana kwa sababu ndiyo inayotutangaza mpaka tunasajiliwa klabu kubwa za Bara hata mimi Yanga waliniona kupitia mashindano hay, Zanzibar kuna wachezaji wazuri lakini namna ya kutoka kucheza soka la mafanikio ndiyo tatizo.

“Siku hizi timu za Bara zinazoshiriki Kombe la Mapinduzi zipo nyingi hivyo, ni fursa ya kipekee kwa wachezaji kupambana na kuonyesha kiwango bora ambapo, baadaye unaweza kusikia timu fulani imesajili huku kupitia haya mashindano,” alisema Ninja ambaye amecheza kwa kiwango bora.