Nafasi nyingine kwa Samatta
Muktasari:
Wapinzani wao hao langoni mwao anasimama kipa mkongwe wa Ivory Coast, Aboubakar Barry.
MWANDISHI WETU
MBWANA Samatta leo Jumamosi anatarajiwa kushuka tena uwanjani wakati timu yake ya Genk itakapokuwa ugenini katika mfululizo wa mechi ya Ligi Kuu Ubelgiji.
Samatta amekuwa haanzishwi na kocha Peter Maes, badala yake aliingizwa dakika 15 za mwishoni katika mechi mbili zilizopita ambapo timu yake iliibuka kidedea.
Leo Jumamosi Genk inayoshika nafasi ya tano kwenye msimamo wa ligi hiyo maarufu kwa jina la Jupiler League, itakuwa ugenini kuvaana na timu iliyo katika nafasi ya 12, Lokeren.
Wapinzani wao hao langoni mwao anasimama kipa mkongwe wa Ivory Coast, Aboubakar Barry.
Timu hiyo pia ina mshambuliaji wa Kibrazili aitwaye Jaja (si yule wa zamani wa Yanga) ambaye katika mechi 14 ametupia mabao matatu.
Katika mechi mbili ambazo Samatta alizoingizwa kucheza dakika 15 za mwishoni, Genk iliibuka na ushindi wa bao 1-0 dhidi ya Mouscron Peruwelz na kuigagadua Waasland Beveren kwa mabao 6-1.
Samatta amekuwa akishukuru hata kupata hizo dakika chache kucheza kwa madai ni kama zinampa uzoefu wa kuizoea ligi hiyo kabla ya kuanza kufanya yake.
Mchezaji huyo anaamini baada ya muda si mrefu, kocha wake atakuwa akimwongezea muda wa kuwapo uwanjani.