Morrison azua hofu Yanga

Morrison bado pasua kichwa Yanga

YANGA inarudi uwanjani leo kumalizana na Zalan ya Sudan Kusini katika mchezo wa marudiano utakaopigwa saa 1:00 usiku katika mechi ya raundi ya awali ya Ligi ya Mabingwa Afrika lakini staa mmoja tu muhimu, Bernard Morrison ‘BM33’ amezusha hofu kubwa kwa benchi la ufundi la timu hiyo.

Tangu Morrison acheze mechi ya mwisho dhidi ya Azam iliyoisha kwa sare ya mabao 2-2, hajaonekana uwanjani tena katika dakika 180 zilizofuata ikiwa ni mechi mbili za mashindano tofauti.

Daktari wa Yanga, Sheicky Mngazija ameliambia Mwanaspoti kuwa, winga huyo raia wa Ghana aliumia katika mchezo dhidi ya Azam, japo ameshapata matibabu na kuona hajapata majeraha makubwa sana.

“Morrison aliumia kifundo cha mguu na tulilazimika kumfanyia vipimo, lakini havikuonyesha kama aliumia sana ila anaendelea vizuri tunaendelea kumfuatilia taratibu kuangalia uimarikaji wake,” alisema Mngazija ambaye ni daktari aliyeitumikia Yanga kwa muda mrefu zaidi.

Wakati Mngazija akifafanua hivyo, kocha Nasreddine Nabi amejikuta akijilaumu kwa hatua ya kumruhusu winga huyo kurudi uwanjani wakati alipopata maumivu dhidi ya Azam.

Morrison aliumia akiwa peke yake na mpira katika dakika ya 89, Yanga ikicheza na Azam alipoukanyaga vibaya mpira kisha kupata maumivu hayo ya kifundo cha mguu na kutibiwa kisha kurejea uwanjani.

“Nilimuuliza utaweza kuendelea akasema ndio, lakini alitaka kurudi baada ya kuona kuna mwenzake Aziz KI (Stephane) ameumia na kama angetoka yeye basi tungeweza kucheza pungufu kama mwenzake angeshindwa kuendelea kwa kuwa tulishakuwa tumekamilisha idadi ya wachezaji wa kubadilisha,” alisema Nabi na kuongeza;

“Tutaendelea kumfuatilia kwa karibu kuona kama atakuwa tayari, hizi sio taarifa nzuri wakati huu ambao tuna mechi nyingi muhimu na hasa ubora wake (Morrison).”

Mbali na mechi ya Zalan iliyoisha kwa Wasudan hao kupigwa mabao 4-0, Morrison alikosa pia pambano la Ligi Kuu Bara dhidi ya Mtibwa Sugar lililopigwa Jumanne na kushinda 3-0.