Mastaa Yanga wauwasha moto

Muktasari:

NANI wa kuuzima moto uliowashwa na mastaa wa Yanga, ambao wamepania kufanya makubwa msimu huu, ikiwemo mipango yao dhidi ya watani wao wa jadi Simba? Mwanaspoti linakupa mchongo mzima wa walichokizungumza.

NANI wa kuuzima moto uliowashwa na mastaa wa Yanga, ambao wamepania kufanya makubwa msimu huu, ikiwemo mipango yao dhidi ya watani wao wa jadi Simba? Mwanaspoti linakupa mchongo mzima wa walichokizungumza.

Baada ya mechi yao na Mbeya Kwanza waliyoichapa mabao 2-0, Uwanja wa Sokoine jijini Mbeya, waliwaahidi mashabiki wao kuyaona makubwa zaidi ya kile walichokifanya kwenye mechi saba zilizopita.

Yanga ndio inayoongoza kwenye msimamo wa Ligi Kuu Bara wakiwa na pointi 19, katika mechi saba ilishinda sita na ilitoka sare dhidi ya Namungo FC.

Kupitia matokeo hayo, staa wa timu hiyo Said Ntibazonkiza ‘Saido’ anayemiliki mabao mawili, alianza kwa kuwaomba radhi mashabiki wa timu hiyo kwa sare waliyoipata dhidi ya Namungo FC, kisha akawapa neno la matumaini.

“Kwanza tunawashukuru mashabiki kwa kuwa bega kwa bega hata tulipopata sare ya bao 1-1 dhidi ya Namungo FC watusamehe kwa hilo, kwani lengo letu lilikuwa ni ushindi, lakini tuwaahidi kwamba hatutawaangusha na watarajie makubwa mbeleni,” alisema.

Aliulizwa ushindi wao dhidi ya Mbeya Kwanza unatafsiri kuelekea mechi yao na Simba. Alijibu “Umetuongezea ari ya kujituma kuhakikisha mashabiki wetu wanacheka kwenye mchezo huo,”

Kauli ambayo iliungwa mkono na Fiston Mayele aliyesema akili zao kwa sasa zinawaza mechi ya Desemba 11 dhidi ya watani zao Simba utakaopigwa Uwanja wa Mkapa.

“Kwasasa tunaelekeza akili zetu kwenye mchezo wa Desemba 11, ili kuhakikisha tunashinda, hilo ndilo lengo letu, kila mchezo kupata pointi tatu,”alisema.