Majirani Derby moto utawaka Zenji leo

New Content Item (1)
New Content Item (1)

Muktasari:

Mchezo huo  awali ulipangwa kuchezwa Machi 2 lakini ulisogezwa mbele baada ya kusimama kwa michezo yote hapa Zanzibar kufuatia kifo cha Rais wa awamu ya pili wa Tanzania, Ali Hassan Mwinyi.

Leo ndio leo. Majirani dabi itapigwa jioni ya leo katika Ligi Kuu ya Zanzibar (ZPL) kati ya Mlandege FC na Kundemba FC kwenye Uwanja wa Mao Zedong A kuanzia saa 10:15 jioni.

Kundemba wao wamesema mara hii wamejipanga kuondoka na alama tatu katika mchezo huo na hawataki yawakute yaliyowakuta mzunguko wa kwanza ambapo wapinzani wao walishinda kwa bao 1-0.

Mchezo huo  awali ulipangwa kuchezwa Machi 2 lakini ulisogezwa mbele baada ya kusimama kwa michezo yote hapa Zanzibar kufuatia kifo cha Rais wa awamu ya pili wa Tanzania, Ali Hassan Mwinyi.

Kocha mkuu wa Kundemba FC, Ali Vuai Shein alisema; “Mashabiki wajitokeze kwa wingi kutuunga mkono wachezaji wana hamasa kubwa na wanaitaka hii mechi, wako kwenye hali nzuri.”

Kocha wa Mlandege FC, Hassan Ramadhan ‘Pele’ ameliambia Mwanaspoti kuwa mechi hiyo ni muhimu kwao kwani wanazihitaji alama tatu ili wazidi kujiweka katika mazingira mazuri ya kuitafuta  Top Four.

Kundemba FC ipo nafasi ya 13 kwenye msimamo ikiwa na pointi 19, wakati Mlandege FC inashika nafasi ya tisa ikiwa na pointi 24.