Lulu amuita kwa mbwembwe Hamisa Mobeto jukwaani
Muktasari:
Msanii Lulu amemuita Hamisa Mobeto kwa kumpamba kila aina ya majina katika tuzo za SZIFF, ambako alikuwa mmoja wa washeherishaji.
Dar es Salaam. Mcheza filamu, Elizabeth Michael 'Lulu' alijikuta akipotezea tofauti alizonazo na mwanamitindo Hamisa Mobeto, kwa kumuita kwa mbwembwe jukwaani.
Lulu alifanya hivyo jana alipokuwa mmoja wa washehereshaji katika tuzo za SZIFF, zilizofanyika usiku wa kuamkia leo February, 24 2019 katika ukumbi wa Mlimani City.
Baadhi ya maneno aliyoyataja Lulu wakati wa kumuita Mobeto ni pamoja na "namleta kwenu model, mrembo, mama wa watoto wawili jukwaani na si mwingine ni Hamisa Mobeto" maneno yaliosababishwa shangwe ukumbini hapo.
Mobeto ni mama wa mtoto wa mchumba wa Lulu, Francis Siza 'Majizo' ambaye awali wakati Majizo alipoanzisha mahusiano na mcheza filamu huyo maarufu hapa nchini, kwa nyakati tofauti walionekana kurushiana maneno ya hapa na pale na Hamisa.
Hamisa naye baada ya kupanda jukwaani aliuonyesha umati uliokuwa umefurika hapo namna gani anaweza kuzungunza Kiingereza kwa ufasaha hali iliyowafanya watu kupiga kelele na yeye kubadili gia angani na kuanza kuongea Kiswahili.
Mrembo huyo ambaye mbali ya uanamitindo, pia ameingia kwenye muziki wa bongo fleva na pia ni muigizaji, alivaa gauni la bega moja la rangi nyeupe na ndiye alikabidi tuzo ya tamthiliya bora amko 'Safari Yangu' iliibuka kidedea.