Kocha mpya Biashara United huyu hapa...

Mwanza. Biashara United imemtambulisha Patrick Odhiambo Okumu kuwa Kocha Mkuu wa timu hiyo akijaza nafasi iliyoachwa wazi na Francis Baraza aliyetimkia Kagera Sugar.

Okumu raia wa Kenya amesaini kandarasi ya miaka miwili kuitumikia timu hiyo ya mjini Musoma mkoani Mara na anatarajia kuanza kazi kuanzia sasa akisaidiana na Marwa Chambeli.

Okumu mwenye leseni B ya Shirikisho la Soka barani Afrika (Caf) atakuwa na kazi ngumu kuendeleza mazuri kikosini humo ikiwa ni kuiwezesha timu kumaliza nafasi nne kwenye Ligi Kuu lakini kuifikisha mbali katika michuano ya Kombe la Shirikisho ambayo kwa sasa wapo robo fainali.

Okumu anajiunga na timu hiyo akitokea klabu ya Kaka Mega Home Boys lakini akizifundisha pia timu kadhaa kama Gor Mahia na Sony Sugar zote za nchini Kenya.

Akizungumza wakati wa kumtamburisha Kocha huyo, Mwenyekiti wa timu hiyo, Seleman Mataso amesema wameamua kumleta Mkenya kutokana na falsafa ya mtangulizi wake, Baraza.

"Tumepokea maombi mengi sana kutoka kwa Makocha tofauti lakini tukaamua kumpitisha Okumu kutokana na falsafa ya mtangulizi wake kuwa nzuri hivyo tunaamini atatufikisha tunapotaka, uongozi utampa ushirikiano tuombe na wadau na mashabiki kuuungana naye" amesema Mataso.