Kocha Kaizer aomba Simba

MCHAKATO wa kusaka kocha mpya wa Simba umefikia patamu baada ya mabosi wa klabu hiyo kuchuja orodha ya majina zaidi ya 100 hadi kufikia10 na sasa wanaisaka tatu bora, huku miongoni mwa walioomba kazi ni Kocha wa zamani wa Kaizer Chiefs, Stuart Baxter.
Mwanaspoti linafahamu, Ofisa Mtendaji Mkuu wa Simba, Barbara Gonzalez ndiye anaendesha mchakato huo wa kuchuja makocha walioomba kazi Msimbazi wengi wakiwa ni kutoka Afrika na Ulaya na baadhi yao wakiwa na majina makubwa.
Katika orodha ya makocha hao walioamba kazi, Barbara amesimamia mchujo wote na sasa wamefika kumi ambao nao watachujwa hadi kubaki watatu na mmoja kati ya hao ndiye atapewa kazi hiyo kwa ajili ya msimu ujao.
Usiku wa juzi Alhamisi Mwanaspoti linafahamu kulikuwa na usaili, iliyotumika saa 1:15 kati ya Barbara na Baxter aliyefutwa kazi miezi miwili iliyopita akiwa Kaizer Chiefs aliyoifikisha fainali ya Ligi ya Mabingwa Afrika msimu uliopita ambapo iliitoa Simba katika robo fainali.
Katika orodha ya makocha 10 Bora waliopo kwenye mchujo mwingine wa kusaka tatu bora na mwishowe kumpata mmoja Baxter alifanyiwa interview hiyo na Barbara kutokana na uwezo wake mkubwa wa kufundisha pamoja na CV yake iliyoshiba.
Katika interview hiyo, inaelezwa Barbara alimuuliza Baxter kama ataweza kuisuka timu hiyo kuwa hatari msimu ujao, kurudisha ubingwa wa Ligi Kuu Bara, Kombe la Shirikisho (ASFC) na Ngao ya Jamii ambayo msimu huu imeyapoteza.
Barbara hakuishia hapo miongoni mwa maswali aliyouliza ni Baxter anaweza kuipa Simba mafanikio kwenye Ligi ya Mabingwa pamoja na mambo mengine ya msingi kwenye maslahi.
Mara baada ya usaili huo Barbara alimueleza Baxter asubiri majibu kama ataingia kwenye orodha ya makocha watatu bora au kupenya moja kwa moja kuchukua mikoba ya Pablo Franco na kama hatafaulu atamueleza pia.
Mbali na Baxter, jina lingine la waliopo 10 Bora ni Msauzi Morena Ramoreboli anayefundisha Jwaneng Galaxy ya Botswana na alikuja hapa nchini akikiongoza kikosi chake kuiondoa Simba kwenye hatua ya mtoano Ligi ya Mabingwa msimu uliyoisha.
Mwanaspoti linafahamu Ramoreboli amepenya kwenye mchujo huo, lakini hatafanyiwa usaili kutokana na kluwa na wasifu (CV) ndogo, pia kushindwa kwake kufanya vizuri kwenye mashindano ya ndani na Afrika lakini Simba si aina ya kocha wanaye muhitaji kwahiyo hatapenya hatua inayofuata na safari yake itaishia hapo.
Katika hatua nyingine jambo la kushangaza kwa uongozi wa Simba na limekuwa likizungumziwa mara kwa mara kwenye mchakato huo wa kutafuta kocha mpya, hakuna hata mzawa mmoja aliyeomba kazi hiyo.
Viongozi hao wa Simba wamekuwa wakizungumza Tanzania kumekuwa na makocha wengi wakubwa wenye resini lakini wanashindwa kuelewa kwa nini hakuna hata mmoja ameshindwa kuomba kazi bila ya kujali kama anaweza kupata au akashindwa.
Katika hatua nyingine Mwanaspoti linafahamu baada ya Barbara kumaliza mwenyewe kufanya mchujo huwa wa makocha na kupata wale watatu wenye sifa ambazo Simba inazihitaji ndio atawasilisha kwa Bodi ya Wakurugenzi kujadili yupi anafaa kumpa kazi.
MSIKIE BARBARA
Alipotafutwa Barbara jana alisema wapo katika hatua nzuri ya kutafuta kocha mpya ambaye atakuja kuifundisha Simba msimu ujao na wapo makini kwenye mchakato huo ili kupata yule mwenye sifa sahihi ambaye wanamuhitaji.
Alisema msimu huu kuna mahala Simba imeshindwa kufanya vizuri na kufikia malengo yake kwahiyo wakipata kocha mzuri atakuja kuitibu hiyo changamoto na kufanya vizuri msimu ujao.
“Kuna makocha wakubwa wenye CV za maana wengine hata sikutegemea kama wanaweza kuomba kazi ya kutaka kuifundisha Simba ila tupo kwenye hatua nzuri na mmoja kati ya hao makocha ndio tutampa kazi namuda ukifika tutamuweka wazi ila kwa sasa bado kutokana mchakato haujakamilika,” alisema Barbara.
WASIFU WA BAXTER
Baxter alianza kufundisha soka, 1985 timu ya Orebro SK, baada ya hapo 1986, alitua IF Skarp, kisha akaenda 1987, Vitoria Setubal mwaka 1988–91, akajiunga na Halmstads BK.
Mwaka 1992–94 alifundisha Sanfrecce Hiroshima kisha 1995–97 alikwenda Vissel Kobe, 1998–00 AIK baada ya hapo 2001 alitua Lyn 1896 FK, mwaka 2002–04, alijiunga na timu ya taifa ya England chini ya miaka 19, baada ya hapo alifundisha timu ya taifa ya Afrika Kusini 2004–05 na mwaka 2006 alitua Vissel Kobe.
Msimu wa 2006–07 alitua Helsingborgs IF, kisha akaenda kufundisha timu ya taifa ya Finland 2008–10 na alijiunga na Kaizer Chiefs kwa mara ya kwanza 2012–15, baada ya hapo 2015, alitua Genclerbirligi.
Msimu wa 2016–17, alitua SuperSport United kisha 2017–19 alirudi tena kuifundisha timu ya taifa Afrika Kusini na msimu 2020–21 alifundisha Odisha na klabu yake ya mwisho ilikuwa Kaizer 2021–22.