Klay sasa njia nyeupe kutisha NBA

Wapenzi wa Ligi ya Kikapu Marekani (NBA) walishuhudia kwa mara nyingine kurejea kwa staa mkubwa, Klay Thompson wa Golden State Warriors akicheza tena baada ya kuwa nje misimu miwili.

Klay Thompson, staa mwenye uwezo mkubwa wa kufunga vikapu vingi kwenye kila mchezo, ikiwemo zile za pointi tatu alikuwa nje kwa miaka hiyo tangu alipocheza mchezo wa sita wa fainali ya NBA 2019 dhidi ya Toronto Raptors.

Tangu acheze mchezo huo hakucheza tena baada ya kuumia na alijaribu kurejea baada ya msimu mmoja na bahati mbaya kwake kabla hajaanza kucheza mechi za ligi alijitonesha mguu na kulazimika kuwa nje mwaka mwingine.

Juzi Jumatatu wachezaji wa Golden State Warriors walivaa jezi namba 11 anayotumia mchezaji huyo kama ishara ya kumkaribisha upya na akacheza kwa dakika 20 na kufunga pointi 17 kwenye mchezo ambao Warriors walishinda kwa pointi 96-82 dhidi ya Clevaland Cavaliers.