Kichuya apiga Hat trick

NYOTA wa Namungo Shiza Kichuya ameingia kwenye vitabu vya kumbukumbu za Ligi Kuu msimu huu baada ya kufunga mabao matatu kwenye mechi moja ‘Hat trick’ dhidi ya Mtibwa Sugar.

Hat trick hiyo imemfanya Kichuya kufikisha mabao nane kwenye ligi msimu huu huku Fiston Mayele wa Yanga na George Mpole wa Geita Gold wakiwa ndio wenye mabo mengi hadi sasa ambapo kila mmoja amecheka na nyavu mara 16.

Kichuya amefunga mabao hayo leo Uwanja wa Manungu dakika ya 23, 50 na 66 katika ushindi wa 4-2 huku bao lingine la Namungo likifungwa na Sixtus Sabilo.

Mabao ya Mtibwa yalifungwa na Steve Nzigamasabo dakika ya tano na George Makang’a dakika ya 10.

Hat trick hiyo inakuwa ya pili kwenye ligi msimu huu na ya kwanza ni ile ya Jeremiah Juma wa Tanzania Peisons aliyofunga Novemba 27 mwaka jana katika uwanja wa Nelson Mandela, Rukwa wakati timu yake ikiiadhibu Namungo kwa mabao 3-1.

Ushindi huo umeifanya Namungo kufikisha alama 40 baada ya mechi 29 huku Mtibwa ikikaa nafasi ya 12 na alama 31 na kila timu imebakiza mechi moja tu kumaliza ligi.