Kazi imeanza, Zoran afyeka watatu Simba

Kazi imeanza, Zoran afyeka watatu Simba

Katika hatua nyingine Kocha Mkuu wa Simba, Zoran Maki amepitisha panga kwa mastraika wawili wa kigeni na kiungo mmoja huku akiwawekea mtegoni wachezaji wengine kikosini.

Taarifa kutoka Misri, zinasema Zoran ametumia siku 13 kuanzia Julai 15, walipoanza kambi akiwasoma wachezaji wake kisha kugundua nani anaweza kuisaidia Simba msimu ujao.

Juzi baada ya Simba kupoteza mchezo wa kwanza, Zoran aliwapa taarifa ya kwanza mabosi akiwaambia hatakubaliana na ubora wa washambuliaji Chris Mugalu na Meddie Kagere. Mbali na Mugalu na Kagere ambao ndio walikuwa washambuliaji wawili pekee wa kigeni walioitumikia Simba msimu uliopita, pia akakata jina la kiungo Thadeo Lwanga.

Tayari jana mastaa hao watatu walipandishwa ndege haraka kurejea nchini kuja kumalizana na mabosi baada ya kocha kuhitaji kubaki na wachezaji wengine pekee. Kilichowashtua zaidi mabosi wa Simba ni kwamba Zoran hajamaliza panga hilo kwani kuna mastaa wengine watatu nao wanaweza kufuata huku mmoja kati ya hao akiwemo nyota mpya kabisa aliyesajiliwa msimu huu.

“Kuna mchezaji mpya katuambia naye hakubaliani na ubora wake lakini tayari tumeshamsajili kwa fedha nyingi hili limetushtua sana tunasubiri,” alisema mmoja wa mabosi wa juu wa Simba.

Habari njema kwa Simba ni kwamba kiungo Sadio Kanoute ambaye alikwama kujiunga na kambi kutokana na pasi yake kujaa yuko katika hatua za mwisho kunjiunga na wenzake akisubiri visa pekee. Kanoute tayari ameshatua Tanzania akisubiri taratibu za safari.