Kaseke kumbe anafanya hivi Yanga

KOCHA Mkuu wa Yanga, Nasreddine Nabi hajakosea kumpanga Deus Kaseke kikosi cha kwanza, kwani staa huyu amesema kila anapopata nafasi, huwa hataki kuondoka uwanjani bure na ameahidi kufunga msimu kwa kishindo endapo Mungu akamjalia afya.

Kaseke alisema anapopewa nafasi ya kuanza kikosi cha kwanza, kuna vitu anavizingatia kabla ya kuanza jukumu lake ili asimwangushe kocha na kuonekana hajapanga mtu sahihi, lakini pia kujua klabu yake inahitaji kitu gani kwa wakati huo na kupandisha thamani ya kazi yake.

Kaseke alisema anapofanya kazi anapenda kujituma zaidi ya alichoagizwa kukifanya uwanjani, mradi tu timu yake ifikie malengo na mashabiki kupata furaha wanayoitarajia kutoka kwao wanapoenda kuwaunga mkono, hivyo anajua wanakuwa wanatumia nauli zao na muda pia.

“Soka linahitaji kujitoa kwanza faida unaipata baadae, ndio maana ninapokuwa uwanjani napenda kucheza kama vile sitakuja kucheza tena, mpira unachezwa eneo la wazi huwezi kudanganya. Kama haupo fiti unaonekana tu,” alisema Kaseke na kuongeza;

“Hutamani sana kila dakika ninayocheza iwe na faida, lakini kwa kuwa mimi ni binadamu kuna wakati siwezi kufikia nitakacho.”